Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia walimu kupata mikopo ya muda mrefu na yenye riba nafuu ili waweze kujenga nyumba bora za kuishi?

Supplementary Question 1

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na juhudi za Serikali ambazo nazipongeza sana lakini ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa Serikali ina mfuko ambao unawapa watumishi wa Serikali mikopo ya muda mrefu ya nyumba, watumishi hao ni pamoja na walimu. Lakini naweza kusema kwamba mfuko huo haupo wazi kwa walimu wote Tanzania na wala kwa watumishi wengine. Je, Serikali imejipanga vipi sasa katika kutoa elimu juu ya mfuko huu ambao unatolewa mikopo yaani mikopo inayotolewa kwa Serikali imejipanga vipi kutoa elimu kwa walimu na watumishi wengine wa Serikali ili waweze kufaidika na mkopo huo wa nyumba wenye gharama nafuu? (Makofi)
Swali la pili; Kwa kuwa Serikali imeonyesha wazi dhamira ya kutaka kuwasaidia walimu na watumishi wengine kupitia Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii lakini mifuko hii inajenga nyumba zenye gharama kubwa sana kuanzia milioni 50 kwenda juu mpaka milioni 75 gharama ambazo mwalimu wa kawaida hawezi kuzimudu.
Je, kwa nini Serikali sasa isiwashawishi Mifuko hiyo ya Jamii ikatoa mikopo ya fedha taslimu kwa walimu waweze kujijengea nyumba zao wenyewe kwa gharama nafuu? Ahsante.

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza alitaka tu tutoe elimu kwa ajili ya walimu kufahamu kwamba kuna mfuko ambao unawawezesha wao kuweza kupata mkopo kwa ajili ya nyumba.
Naomba niseme kwamba mfuko huu tulionao Serikalini siyo kwa ajili ya walimu tu, ni mfuko kwa ajili ya watumishi ambao wanaweza kukopeshwa kupitia mfuko wa Serikali.
Kwa hiyo, elimu ambayo tunaweza kuitoa ni pamoja na sisi wenyewe Wabunge kuweza kutoa elimu hii katika Halmashauri zetu kupitia vikao vyetu vya Mabaraza ya Madiwani ili waweze kuwafahamisha pia walimu huko waliko pamoja na watumishi wengine wa kawaida kwamba wanaweza wakapata fursa hiyo kupitia Serikalini. Kwa hiyo, hili ni la kwetu tumelichukua pamoja lakini tushirikiane wote ili kuweza kufikisha ujumbe huu.
La pili, dhamira ya hizi Hifadhi za Jamii katika ujenzi wa nyumba anasema zina gharama kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba nimezungumzia suala la Watumishi Housing ambalo ni Shirika ambalo limeanzishwa na Mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii na Shirika hili linatoa nyumba zake kwa gharama nafuu wala hazina gharama kubwa sana isipokuwa masharti yake yalipo ni lazima kwanza uwe na dhamana ambayo inaweza ikakusaidia katika kuweza kurudisha mkopo ule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia mabenki yale ambayo yanatoa mkopo huu once ukishakubaliana na benki kwamba sasa unataka kuchukua mkopo, Shirika ndiyo linawasiliana na wewe katika hali halisi ya kutaka kujenga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninachotaka kusema ni kwamba nyumba zinazojengwa ziko katika size mbalimbali, kwa hiyo bei ya nyumba na gharama yake itategemea pia na ukubwa wa nyumba. Kwa hiyo, tunapokuwa na mashirika mengi yanayofanya shughuli za ujenzi, ushindani utakuwepo lakini na ubora wa nyumba utakuwepo. Kwa hiyo, itakuwa ni juhudi ya mtu mwenyewe na kuweza kuchagua ni shirika lipi unataka wewe likujengee nyumba katika gharama ile ambayo unaweza, lakini nyumba ziko za gharama nafuu kulingana na vipato vya wananchi wetu.

Name

Stanslaus Shing'oma Mabula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nyamagana

Primary Question

MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia walimu kupata mikopo ya muda mrefu na yenye riba nafuu ili waweze kujenga nyumba bora za kuishi?

Supplementary Question 2

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ningependa tu kufahamu kutoka kwa Mheshimiwa Waziri kwamba pamoja na mikakati hii mizuri ambayo Serikali inayo katika kuwasaidia watumishi wakiwemo Walimu kupata mikopo ya muda mrefu, sasa ni lini Serikali itazishauri au itazielekeza hizi Halmashauri zetu zote nchini kuhakikisha kwamba kila zinapofanya zoezi la upimaji wa ardhi Walimu wanapewa kipaumbele katika kupata maeneo ambayo pamoja na mkopo watakaopata basi ardhi isiwe kikwazo kwao na waweze kumudu ujenzi huu wa sasa? Nakushukuru sana.

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake anataka kujua ni lini Walimu watapewa kipaumbele kuweza kupewa viwanja pale ambapo Halmashauri zinapima. Ninachoweza kusema tu ni kwamba mipango ya upimaji katika Halmashauri zetu tunaiandaa wenyewe katika vikao vyetu. Kwa hiyo, katika kutoa vipaumbele kwenye kupima, nadhani kwa sababu tumeona kwamba Walimu wana tatizo kubwa ni jukumu letu pia kuhakikisha kwamba tunapopima maeneo basi tunatenga kwa ajili ya watumishi na si Walimu tu kama ambavyo tunavyofanya katika Wizara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo pale ambapo panakuwa pana hitaji kubwa, ni jukumu letu sisi wenyewe kuweza kusema sasa tunapima viwanja sehemu fulani tunawapa watumishi. Kwa upande wa Mwanza, tayari kuna viwanja zaidi ya 500 ambavyo vilipimwa kwa ajili ya watumishi wote kwa ujumla na sio Walimu tu. Kwa hiyo hii inawezekana inaweza kufanyika, ni mipango ya Halmashauri husika.