Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Halima Ali Mohammed

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HALIMA ALI MOHAMMED aliuliza:- Wasichana wanaohitimu kidato cha sita wanakuwa na ufaulu mzuri lakini wanapojiunga na vyuo vya elimu ya juu ufaulu wao huanza kushuka hadi wengine hufikia kusimamishwa masomo kwa sababu ya ufaulu hafifu. Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wasichana katika elimu yao ya juu ili ufaulu wao uweze kuongezeka na kufikia malengo yao?

Supplementary Question 1

MHE. HALIMA ALI MOHAMMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri.
Kwa kuwa kuna malalamiko makubwa yanayohusiana na kubainika kwamba kuna rushwa ya ngono katika vyuo vyetu, jambo ambalo linapelekea wasichana wengi kupata ufaulu mdogo, lakini vilevile wasichana wengine kutoroka shule, lakini kama haitoshi kuna wasichana ambao wamefanya maamuzi ya kujiua na ushahidi upo. Sasa je, Serikali ina mkakati gani wa kufanya utafiti ni kiasi gani wasichana wameathirika na rushwa ya ngono?(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba wasichana wetu wanapatiwa elimu kuhusiana na rushwa ya ngono?

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli taarifa hizo za rushwa za ngono zimekuwa zikisikika na hata hivi karibuni ilijitokeza taarifa ya aina hiyo kwa mwalimu mmoja ambaye ameendelea kuchukuliwa hatua na niseme tu kwamba suala la kufanya utafiti ni suala jema, mimi nichukulie kwamba ntalichukua ili kujifunza tatizo hilo kwa undani zaidi. Lakini niwaombe pia wanafunzi wa kike kutoa ushirikiano, lakini pia hata wanafunzi wa kiume wanaweza kusaidia kutoa ushirikiano kwa mambo ambayo yanajitokeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili katika suala la elimu, sisi wenyewe tumekuwa tukiongea na wanafunzi kupitia wakati tofauti tofauti tunapowatembelea, lakini pia nafahamu kuna taasisi mbalimbali zinazoshughulika na masuala ya kijinsia zimekuwa zikiendelea kuelimisha. Niwaombe pia hata Waheshimiwa Wabunge mnapopata nafasi muweze pia kuongea na wasichana hao ili kuweza kusaidiana kwa pamoja kuona kwamba wote tunakuwa pamoja katika kupigana na kupambana kwamba rushwa za ngono zisipatikane katika shule na hata katika maeneo ya kazi.

Name

Kasuku Samson Bilago

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Buyungu

Primary Question

MHE. HALIMA ALI MOHAMMED aliuliza:- Wasichana wanaohitimu kidato cha sita wanakuwa na ufaulu mzuri lakini wanapojiunga na vyuo vya elimu ya juu ufaulu wao huanza kushuka hadi wengine hufikia kusimamishwa masomo kwa sababu ya ufaulu hafifu. Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wasichana katika elimu yao ya juu ili ufaulu wao uweze kuongezeka na kufikia malengo yao?

Supplementary Question 2

MHE. KASUKU S. BILAGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Suala la ufaulu wa watoto wa kike elimu ya juu inategemea na ufaulu wa watoto haohao wa kike kwenye shule za chini (O-Level na A-level), sasa kumekuwa na tatizo la watoto wa kike wanaobeba mimba wakiwa shuleni kuachishwa masomo, na hili tumekuwa tukilizungumza muda mrefu; ni lini Serikai italeta utaratibu hapa Bungeni, sheria itungwe ili watoto wa kike wanaobeba mimba shuleni wakishajifungua waruhusiwe kuendelea na shule?

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hilo limezungumziwa katika nyakati tofauti tofauti, hivi karibuni pia tulipitisha mpango wa kushughulikia masuala yoyote yanayohusika na unyanyasaji kwa watoto wa kike na suala hilo limekuwa likishughulikiwa mia na Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu na tayari rasimu ya mwanzo ya mwongozo imeshatoka namna gani tufanye na pia niliweza kwenda kutembelea Zanzibar kuongea na Mheshimiwa Waziri kule kuweza kujua wenzetu wamekuwa wakifanya vipi katika eneo hilo, tukajifunza changamoto ambazo zilikuwa zinajitokeza kwa upande wao kwa mfano mwingine anaweza akasema anapata mimba na aliyempa mimba akasema anataka kumuoa katika mazingira kama hayo. Lakini mwisho wa yote tunaamini kwamba tutaweza kutekeleza kuona kwamba fursa zinatolewa kwa mtoto wa kike aliyepata mimba kuweza kurudi shuleni.
Changamoto tu ni namna gani, je arudi kwenye shule ileile, je unyanyapaaji utakuwepo au apewe shule maalum, ndiyo hayo ambayo wadau mbalimbali wanaendelea kutoa mawazo lakini mwisho wa yote tutatekeleza mapema iwezekanavyo.

Name

Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HALIMA ALI MOHAMMED aliuliza:- Wasichana wanaohitimu kidato cha sita wanakuwa na ufaulu mzuri lakini wanapojiunga na vyuo vya elimu ya juu ufaulu wao huanza kushuka hadi wengine hufikia kusimamishwa masomo kwa sababu ya ufaulu hafifu. Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wasichana katika elimu yao ya juu ili ufaulu wao uweze kuongezeka na kufikia malengo yao?

Supplementary Question 3

MHE. AMINA S. MOLELL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Katika vyuo vikuu suala la miundombinu kwa watu wenye ulemavu ni tatizo, na mfano katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ni moja ya changamoto inayochangia wanafunzi wengi hasa watoto wa kike katika kwenda madarasani na hata katika suala zima la mitihani ni tatizo kwao kutokana na changamoto mbalimbali zilizopo. Je, Serikali inatoa kauli gani na hasa kwa kuzingatia chuo hiki ni kikongwe, lakini mpaka leo miundombinu bado ni tatizo na ni kikwazo kwa watu wenye ulemavu?

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa mujibu wa sera kwa ajili ya watu wenye ulemavu, inazungumzia kuwawekea mazingira bora ya kujifunzia na kufundishiwa. Kwa hali ya sasa ni kwamba tunayo majengo ambayo yamejengwa zamani na unakuta kweli yana changamoto ya miundombinu, lakini tunachofanya ni kwamba tunashauri madarasa yale yenye wanafunzi wenye ulemavu wahakikishe yanakuwa ni yale yanayofikika, kwa mfano kama darasa lina mwanafunzi mwenye ulemavu ni vyema likachaguliwa lile ambalo liko katika ground floor ili mwanafunzi yule aweze kufika darasani bila usumbufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa majengo yote mapya yanayojengwa tumeagiza kwamba lazima kila jengo liwekewe miundombinu inayomuwezesha mtu mwenye ulemavu kufikia katika eneo lolote analohitaji kuishi au kujifunzia na hivyo imekuwa ikifanyika na ni rai yangu kusema kwamba hata hiyo miundombinu inayowekwa kwa ajili ya watu wenye ulemavu iwe ni ile inayozingatia viwango vinavyohusika, kwa sabau sasa hivi unakuta kwamba kuna shule zinapokaguliwa ili zionyeshe miundombinu yenye ulemavu zinaweza zikaonesha tu kwamba kuna lile tuta (rump) limewekwa pale lakini unakuta jinsi ambavyo limewekwa lina msimamo mkubwa kiasi kwamba hata huyo mtu mwenye ulemavu anapata shida, kwa hiyo lazima kuzingatia viwango vinavyohusika katika kuweka miundombinu ya watu wenye ulemavu ikiwemo kuweka lifti. ahsante.