Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Lucia Ursula Michael Mlowe

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:- Jeshi la Zimamoto Mkoani Njombe linakabiliwa na ukosefu wa Ofisi pamoja na vitendea kazi hususan magari jambo linalopelekea Jeshi hilo kushindwa kufanya kazi kwa ufanisi. Je, ni lini Serikali italipatia Jeshi hilo ofisi za kudumu pamoja na magari ili liweze kutoa huduma nzuri kwa wananchi?

Supplementary Question 1

MHE. LUCIA M. MLOWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli sijaridhika kabisa na majibu ya Naibu Waziri, Jeshi la Zimamoto linafanya kazi katika mazingira magumu sana. Mfano, Mkoa wangu wa Njombe hawana ofisi, wanatumia majengo ya Idara ya Maji, hawana magari; na tukiangalia Mkoa wa Njombe kijiografia umekaa vibaya sana na matukio ya moto ni mengi.
Nilikuwa nataka kujua time frame, ni lini Serikali itatoa vifaa au vitendea kazi kwa Jeshi la Zimamoto?
Swali langu la pili, kwa kuwa huduma ya Zimamoto iko zaidi mijini, lakini matatizo ya moto yako mengi sana vijijini. Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha hata watu wa vijijini wanapata huduma hii? Ahsante.

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi kwamba tuna matatizo ya ofisi pamoja na vitendea kazi nchi nzima kwa Jeshi la Zimamoto; na ukiangalia katika Wilaya zote takribani za nchi nzima kwa upande wa Tanzania Bara ni Wilaya 20 ambapo kuna Ofisi za Zimamoto mpaka sasa hivi pamoja na magari.
Hata hivyo, Serikali imefanya jitihada kubwa sana kuhakikisha kwamba tunatanua wigo ili huduma hizo ziweze kufika mpaka vijijini na ndiyo maana tuna mpango sasa hivi wa kuhakikisha kwamba tunapeleka huduma za Zimamoto katika Wilaya zote nchini hatua kwa hatua kwa kuanza kupeleka Maofisa ili waweze kutoa elimu na baadaye kadri vifaa vitakavyopatikana tutapeleka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na magari pamoja na vitendea kazi, katika bajeti ya mwaka huu tumetenga takriban shilingi bilioni 1.5 kununua magari mawili, tutaangalia ni maeneo gani ya kipaumbele tuweze kupeleka.
Naomba nichukue fursa hii kumwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutashauriana na Makao Makuu Idara ya Zimamoto tuone uharaka wa kufanya hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tuna mpango mwingine, tunafanya mazungumzo sasa hivi na Austria pamoja na Belgium, Kampuni ya SOMAT ya Belgium ili kuweza kupata mkopo wa Euro bilioni tano pamoja na Euro milioni 1.9 ambazo zitasaidia kuweza kununua vifaa viweze kupunguza makali ya upungufu wa vifaa katika maeneo mbalimbali nchini mwetu.

Name

Freeman Aikaeli Mbowe

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Hai

Primary Question

MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:- Jeshi la Zimamoto Mkoani Njombe linakabiliwa na ukosefu wa Ofisi pamoja na vitendea kazi hususan magari jambo linalopelekea Jeshi hilo kushindwa kufanya kazi kwa ufanisi. Je, ni lini Serikali italipatia Jeshi hilo ofisi za kudumu pamoja na magari ili liweze kutoa huduma nzuri kwa wananchi?

Supplementary Question 2

MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Mambo ya Ndani inakabiliwa na upungufu mkubwa wa magari na ninamshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kukiri kwamba wanapungukiwa sana magari, vitendea kazi pamoja na ofisi. Vilevile wana upungufu mkubwa wa rasilimali watu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali langu, siku za karibuni, kwenye upande wa Jeshi la Polisi ndani ya Wizara ya Mambo ya Ndani pamejitiokeza utaratibu ambapo Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wanalitumia Jeshi la Polisi kuwalinda wao binafsi wakati kuna matatizo makubwa ya kiulinzi katika Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali langu ni hili, nikitoa mifano halisi, katika Mkoa wa Arusha, Mkuu wa Mkoa wa Arusha analindwa na section nzima ya Jeshi la Polisi, ana motorcade, ana ving‟ora asubuhi mpaka usiku. Sasa magari kama mawili au matatu yanamhudumia Mkuu wa Mkoa na section nzima ya Jeshi la Polisi ambayo ina askari tisa na ving‟ora na hata Wakuu wa Wilaya wamejipa utamaduni huo sasa.
Je, ni nini itifaki ya Kitaifa kuhusu ulinzi wa Viongozi kama hata hawa Mawaziri wenyewe hawalindwi na Askari, lakini Wakuu wa Mikoa leo wanajilundikia Askari badala ya Askari kwenda kwenye lindo, ma-OCD wote siku hizi hawafanyi kazi ya ulinzi wanafanya kazi ya kulindana na kufuatana na Wakuu wa Wilaya. Tunaomba Wizara watueleze leo, ni nini sera ya Serikali kuhusu itifaki hii na matumizi mabaya ya Jeshi la Polisi?

Name

Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwenye utendaji wa kazi kwenye ngazi za Mikoa na Wilaya, Mkuu wa Mkoa ni Mwenyekiti wa Ulinzi na Usalama wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya ni Mwenyekiti wa Ulinzi na Usalama wa Wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, panapokuwepo na jukumu hasa ambalo linapohusisha shughuli za kiulinzi na nje ya ofisi, ni sahihi Mkuu wa Mkoa ama Mkuu wa Wilaya kuambatana na timu yake kwenda katika eneo husika. Inapotokea Mkuu wa Mkoa anakwenda ofisini kwake ama Mkuu wa Wilaya anakwenda ofisini kwake, maana yake OCD ama RPC ama wengine na wenyewe watakuwa kwenye ofisi zao. (Makofi)
Kwa hiyo, mimi kwa mazingira ambayo nimekuwa nikipewa ni pale ambapo hawa viongozi wanakwenda katika eneo la tukio ambalo linahusisha ulinzi na usalama. Huo ndiyo muogozo kwamba kama wanaelekea katika eneo ambalo linahusisha ulinzi na usalama ni sahihi viongozi hawa kwenda na timu zao kwa sababu ni mambo ya kiusalama na sehemu ya kutolea maelekezo, lakini siyo wakati wa kwenda ofisini on daily routine, unless kama wanafanya hivyo itakuwa maeneo ambayo kila mmoja anaenda kwenye ofisi na ofisi hizo ziko katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, kwa maelekezo haya, ni kwamba viongozi hawa wanapokwenda kwenye majukumu ambayo yanahitaji maelekezo na ni ya kiulinzi na usalama na wao ndio Wenyeviti wa Ulinzi na Usalama itifaki inataka hawa watu wawe na hao viongozi kwa ajili ya maelekezo ya site, lakini wanapoenda kazini na hawa viongozi wengine nao wanaendelea na majukumu yao.