Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

John Wegesa Heche

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Tarime Vijijini

Primary Question

MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:- Kwa mujibu wa tafiti, uchimbaji mdogo ndio unaotoa ajira kwa wingi katika sekta ya madini:- (a) Je, ni lini Serikali itajenga maeneo maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo katika eneo la Nyamongo? (b) Je, kwa kutokuwatengea vijana maeneo ya uchimbaji, Serikali haioni kuwa inazidisha chuki ya vijana dhidi ya mgodi wa Acacia North Mara?

Supplementary Question 1

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya watu wa Tarime.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna utofauti wa uelewa wa wachimbaji wadogo kati ya uelewa walionao Serikali na uelewa tulionao sisi wananchi na tunaokaa maeneo ya migodi. Tunapozungumzia wachimbaji wadogo, hatuzungumzii watu wajanja wajanja wanaoweza kwenda mjini wakapata leseni, wakarudi wakajiita wachimbaji wadogo. Tunazungumzia watu waliopo kule kijijini ambao ndio wanachimba kwa kutumia majembe, sururu na nyenzo nyingine ambazo ni duni.
Sasa swali langu, kuna maeneo ambayo yalikuwepo na watu wanachimba pale na bahati mbaya watu wanatoka kule vijijini wanakwenda Dar es Salaam wanapewa leseni, Serikali haishirikishi hata Serikali za Vijiji, wanarudi wanaondoa wachimbaji wadogo, kama eneo moja linaitwa Tigite, bwana mmoja ameondoa zaidi ya watu 20 pale. Sasa nataka Naibu Waziri anijibu, ni lini Serikali itatenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo walioko kule vijijini, sio hawa wenye leseni wanaokwenda Dar es Salaam? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wakati Mgodi wa North Mara unaanza, ulitwaa eneo kwa maana ya ile leseni waliyopewa, walipewa eneo kubwa sana na kuna maeneo ambayo mpaka sasa hawayatumii na hawayafanyii kazi. Mojawapo ya eneo hilo ni Serengeti Crossing. Kwa nini Serikali isiuombe mgodi utoe lile eneo kwa wananchi kwa sababu mgodi haulitumii kabisa, ili wananchi wafanye kazi pale wajipatie kipato na waendeshe maisha yao?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Heche jinsi ambavyo ameendelea kutupa ushirikiano katika masuala mbalimbali ya migogoro ya wananchi wa Nyamongo. Nakupongeza sana Mheshimiwa Heche. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hayo, nijielekeze kwenye maswali yake ya nyongeza, ni lini Serikali itatenga maeneo katika maeneo mengine hasa katika eneo la Tigite ambalo amelitaja? Naomba tu mara baada ya kikao hiki nikutane na Mheshimiwa Heche atupatie maeneo kwa sababu Serikali bado inaendelea kuongea na mgodi ili ipate maeneo mengine kwa wachimbaji wadogo. Kwa hiyo, nitazungumza na Mheshimiwa Heche kuhusiana na hili ili eneo la Tigite alilotaja pia litengewe wananchi wa Nyamongo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na swali lake la pili, kwanza tu nieleze kwamba Mheshimiwa Heche anavyosema kwamba North Mara imepewa maeneo makubwa, ni kweli, yapo maeneo ambayo Serikali inazungumza na mwekezaji ambayo ni makubwa na mgodi haujaanza kuyatumia. Tunafanya majadiliano, yakishakamilika, tutaongea na Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, kabla leseni hazijatoka, utaratibu tulioweka sasa ni pamoja na kushirikisha viongozi wa maeneo yale ili leseni itakapotoka waweze kutupa ushirikiano mkubwa. Kwa hiyo, eneo hili ambalo ni kubwa kwa wachimbaji wakubwa, tutazungumza na Mgodi wa North Mara, maeneo ambayo tutayapata Mheshimiwa Heche tutashirikiana na wewe ili wananchi waendelee kupelekewa maeneo zaidi.

Name

Tundu Antiphas Mughwai Lissu

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Singida Mashariki

Primary Question

MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:- Kwa mujibu wa tafiti, uchimbaji mdogo ndio unaotoa ajira kwa wingi katika sekta ya madini:- (a) Je, ni lini Serikali itajenga maeneo maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo katika eneo la Nyamongo? (b) Je, kwa kutokuwatengea vijana maeneo ya uchimbaji, Serikali haioni kuwa inazidisha chuki ya vijana dhidi ya mgodi wa Acacia North Mara?

Supplementary Question 2

MHE. TUNDU A. M. LISSU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Naomba kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri swali la nyongeza linalofanana na swali ambalo ameuliza Mheshimiwa John Heche.
Mheshimiwa Naibu Spika, jimboni kwangu kuna eneo lina dhahabu na kampuni moja inaitwa Shanta Mining imeingia na kupewa eneo hilo tangu mwaka 2004. Leo ni miaka 13 haijaanza kuchimba madini, haijajenga mgodi na kwa taarifa za kitaalam ambazo nimeziangalia, hizo deposits za dhahabu siyo kubwa sana za kuweza kupewa kampuni ya kigeni. Namwomba Mheshimiwa Naibu Waziri alieleze Bunge lako kama Serikali ina mpango wa kulitwaa hilo eneo na kuwarudishia wananchi ili wachimbaji wadogo wadogo wenyeji wachimbe kwa sababu baada ya miaka 13 hawachimbi, hawa wawekezaji inaelekea hawana mpango au uwezo wa kuchimba dhahabu kwenye hili eneo la Mang‟oni.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, kwanza namshukuru Mheshimiwa Tundu. Nimekuwa nikiwasiliana naye mara kwa mara kuhusiana na kumpatia eneo. Niseme tu, ni kweli kabisa Kampuni ya Shanta Mining ilipewa leseni ya utafiti tangu mwaka 2004. Nieleze kidogo, muda wa kufanya utafiti kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya 2010, awali ya kwanza ni miaka minne, baada ya miaka minne anapewa tena miaka mitatu ya kuendelea na utafiti na hatimaye anamalizia miaka mitatu. Kwa hiyo, ni kweli kabisa shughuli za utafiti zinachukua muda mrefu. Hilo la kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, baada ya kukamilisha utafiti, kampuni inatakiwa ianze shughuli za uchimbaji, hivi sasa kama ambavyo Mheshimiwa Tundu anasema haijaanza, matarajio ya mgodi ni kuanza shughuli za uchimbaji kati ya Juni, 2018. Kwa hiyo, baada ya shughuli za uchimbaji kuanza, basi maeneo mengine yata maeneo mengi yatashughulikiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia yapo maeneo ambayo Kampuni ya Shanta Mining tunazungumza nayo. Hivi sasa tumezungumza na Kampuni ya Shanta Mining, inatarajia kuwa na maeneo ya hekta kama 200 ambayo inaweza ikawaachia wananchi wa Singida ili wachimbe kwa ajili ya uchimbaji mdogo kwa sababu yanaweza kuonekana siyo manufaa kwa kampuni hiyo. Baada ya taratibu hizo kukamilika, Mheshimiwa Tundu Lissu basi wananchi wako watawasiliana na Serikali tu na watapewa maeneo hayo.

Name

Joseph Kasheku Musukuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita

Primary Question

MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:- Kwa mujibu wa tafiti, uchimbaji mdogo ndio unaotoa ajira kwa wingi katika sekta ya madini:- (a) Je, ni lini Serikali itajenga maeneo maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo katika eneo la Nyamongo? (b) Je, kwa kutokuwatengea vijana maeneo ya uchimbaji, Serikali haioni kuwa inazidisha chuki ya vijana dhidi ya mgodi wa Acacia North Mara?

Supplementary Question 3

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa wananchi wa Geita walipewa magwangala fake, na kwa kuwa Sheria ya Leseni ya Uchimbaji Mkubwa inawataka wachimbaji wakubwa kila baada ya miaka mitano wamege baadhi ya eneo wawarudishie wachimbaji wadogo. Je, Wizara iko tayari sasa kulimega eneo la Nyamatagata na Samina kuwarudishia wananchi kuwafuta machozi kwa magwangala fake waliyopewa?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa namshukuru Mheshimiwa Musukuma, katika jitihada ambazo ziliwasababisha wananchi wapewe magwangala ni pamoja na Mheshimiwa Mbunge. Kwa hiyo, tunakupongeza Mheshimiwa Musukuma. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitambue kwamba shughuli za utafiti na uchimbaji wa madini kwa kawaida kabisa, ni za kupata na kupotea. Sasa ni jambo la kawaida, mwekezaji anaweza akawekeza kwenye kuchimba na akakosa. Kama ambavyo ilikuwa kwenye magwangala, wananchi walitarajia pangekuwa na thamani, lakini bahati mbaya hapakuwa na thamani. Kwa hiyo, nilitaka tu kumwelewesha Mheshimiwa Musukuma na ninampongeza sana. Pia kwa wachimbaji wote, ni jambo la kawaida mchimbaji kuanza kuchimba na asipate madini ya thamani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba tu kusema, suala la Nyamatagata na Samina, ni kweli kabisa Serikali inazungumza na Mgodi wa GGM pamoja na wawekezaji wengine, hivi sasa tuko katika hatua nzuri. Mwaka 2016 Kampuni ya GGM ilirusha ndege kuangalia maeneo ambayo hayahitaji.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Musukuma nikuhakikishie kwamba mara baada ya taratibu hizi kukamilika, wananchi wa Nyamatagata na Samina, maeneo ambayo yataachiwa na mgodi, basi yatatengwa rasmi kwa ajili ya wananchi, lakini baada ya kukamilisha mazungumzo na mgodi.

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Primary Question

MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:- Kwa mujibu wa tafiti, uchimbaji mdogo ndio unaotoa ajira kwa wingi katika sekta ya madini:- (a) Je, ni lini Serikali itajenga maeneo maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo katika eneo la Nyamongo? (b) Je, kwa kutokuwatengea vijana maeneo ya uchimbaji, Serikali haioni kuwa inazidisha chuki ya vijana dhidi ya mgodi wa Acacia North Mara?

Supplementary Question 4

MHE. HUSSEIN M. BASHE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Na mimi naomba kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa wananchi wa maeneo mengi ambayo wawekezaji wakubwa wamewekeza wameacha athari kubwa katika maeneo hayo na mojawapo ni Wilaya ya Nzega katika Mgodi wa Resolute, wananchi wameachiwa mashimo makubwa bila manufaa yoyote. Je, Serikali sasa iko tayari kumnyima mwekezaji Kampuni ya Resolute, certificate ya kumruhusu kuondoka nchini ambayo anatakiwa apewe mwezi wa sita kabla hajalipa deni ambalo anadaiwa la shilingi bilioni 10 na Halmashauri ya Mji wa Nzega?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa Kampuni ya Resolute ilifunga mgodi wake miaka mitatu iliyopita. Katika utaratibu wa uchimbaji, mgodi unapoanza huwa kuna Mine Closure Plan. Kwa hiyo, wakati wanafunga mradi, kampuni ilitakiwa kutekeleza Mine Closure Plan, lakini sambamba na hilo, huwa inapewa certificate ya ku-close mgodi. Sasa Wizara ya Mazingira pamoja na NEMC wanalifanyia kazi suala hilo, watakapokamilisha taratibu Mheshimiwa Bashe utashirikishwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la msingi ni kwamba je, ni kwa nini Serikali haioni sababu ya kuwanyima certificate? Ni jambo ambalo namwomba Mheshimiwa Bashe avute subira, watu wetu wa NEMC na Mazingira wanalifanyia kazi. Nitambue ushiriki wako Mheshimiwa Bashe kwa wananchi wa Nzega. Niseme tu sambamba na hilo, ili kuwawezesha wananchi wa Nzega wapate maeneo na kuondokana na athari, mara baada ya taratibu za mazingira kukamilika, maeneo ambayo yaliachwa na Resolute ambayo yako wazi, yatamilikishwa kwa wananchi wako ili waweze kupata shughuli za kufanya kazi.