Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Rwegasira Mukasa Oscar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Primary Question

MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:- Matumizi yasiyo sahihi ya lugha ya Kiswahili kwenye vyombo vya habari hayatoi fursa ya kukua kwa lugha yetu na badala yake yanachangia kurithisha lugha yetu kwa watoto kwa namna iliyo mbovu; mathalani, Mtangazaji wa runiga au redio anasema “hichi” badala ya “hiki” au nyimbo hii badala ya “wimbo huu” na kadhalika. Je, Serikali ina mpango gani wa kimkakati wa kuvifanya vyombo vya habari kuwa mawakala wa kulinda usahihi wa lugha ya Kiswahili badala ya kuwa miongoni mwa wabomoaji wa lugha yetu?

Supplementary Question 1

MHE. OSCAR R. MUKASA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nina maswali mawili ya nyongeza. Upo ushahidi wa matumizi yasiyo sahihi ya lugha ya Kiswahili miongoni mwa viongozi wa Serikali na miongoni mwetu Wabunge. Kwa sababu Bunge na viongozi wa Serikali ni miongoni mwa makundi ya jamii na taasisi zenye wajibu wa juu kabisa wa kulinda lugha hii na kwamba inaashiria tatizo hili haliko kwenye vyombo vya habari tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, je, Serikali inasema nini kuhusu upana wa tatizo hili hasa kwa wakati huu ambapo inatengeneza sera hiyo?
Pili, kwa sababu matumizi, kwa mfano ya neno “hichi” badala ya “hiki,” “nyimbo hii” badala ya “wimbo huu,” uchanganyaji wa lugha ya Kiingereza kwa kiwango kilichokithiri kwenye sentensi za Kiswahili, vinakera. Tunaomba kujua ni lini sera hii inakuja kudhibiti hali hii inayoendelea? Nakushukuru.

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Oscar Mukasa, Mbunge wa Biharamulo kwa jinsi ambavyo amejitahidi kuonesha ukinara katika kuikuza lugha ya Kiswahili. Naomba kujibu maswali yake mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kumekuwepo na matumizi ambayo siyo sahihi ya lugha yetu ya Kiswahili na wengi tumekuwa tukishuhudia kwa mfano “hiki kikao” wengine husema “hichi kikao,” “hiki kitu”, “hichi kitu” na pengine kama alivyosema katika maelezo yake kwenye swali lake la msingi, ni kwamba hata watoto kwa sasa ukifuatilia utaona, “hiki kitu” kwa sababu tunatumia “hichi kitu,” sasa na wao wameanza kusema “hiko kitu.” Wameibadilisha, badala ya “hiki kitu,” sasa wanasema “hiko kitu.”
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile siyo katika Kiswahili tu, watu wamekuwa wakichanganya Kiingereza, lakini hata lugha zetu za asili vilevile wamekuwa wakichanganya Kiingereza. Kwa mfano, unaweza kumsikia mtu anasema “infact kwa kweli angambila nshomile.” Haya ni maneno ambayo yamekuwa yakichanganywa katika lugha za asili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wito wa Serikali ni kwamba tulinde Kiswahili na pia tulinde lugha zetu za asili kwa sababu zile lugha za asili ndipo tunapoweza kupata maneno ya kuongeza kwenye Kiswahili pale ambapo tutakuwa hatuna maneno mbadala ya Kiingereza. Kwa hiyo, tulinde lugha zetu zote, lugha ya Kiswahili na pia lugha ya asili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuongezea tu ni kwamba Serikali ipo tayari kupitia BAKITA kuja kutoa semina katika Bunge hili ili kusudi tuweze wote kwa pamoja kufuatilia na kutumia lugha ya Kiswahili kwa ufasaha. Nalisema hili kutokana na kwamba kuna visababishi ambavyo vinapelekea matumizi yasiyo sahihi au visababishi ambavyo vinaweza kumwezesha mtu atumie lugha ya Kiswahili kwa ufasaha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, katika nchi za Afrika Mashariki wanaotumia lugha ya Kiswahili kama lugha ya asili ni watu wapatao milioni mbili hadi milioni 15 kwa mujibu wa takwimu. Lakini wengi wao kuanzia milioni 50 hadi milioni 150, wengi wanatumia Kiswahili kama lugha ya pili. Kwa hiyo, wakati mwingine inatokea tafsiri ya lugha zile za asili kwa Kiswahili.
Vilevile kuna kisababishi kingine ambacho ni jinsi gani ile lugha ya asili inashabihiana na lugha ya Kiswahili. Kwa mfano, Kiswahili kina „r‟ na kina “l” lakini zipo lugha ambazo hazina „r‟ na hazina „l‟. Kwa mfano, kuna lugha moja ya asili isiyokuwa na „r‟, akitaka kusema „anataka kula‟ anasema „nataka kura‟ na mwingine akisema naomba kura anasema „naomba kula.‟ Kwa hiyo, hivi ni visababishi ambavyo vinapelekea matumizi sahihi au yasiyo sahihi kwa lugha ya Kiswahili.
Jambo lingine ni dhamira ya mtu ya kutaka kuwa kinara katika kutumia lugha ya Kiswahili. Kwa mfano, tunavyomwona Mheshimiwa Rwegasira, yeye ana dhamira ya kutakakuwa kinara. Kwa hiyo, nawaomba Waheshimiwa Wabunge na viongozi tuwe na hii dhamira.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni ile tabia ya kujisomea vitabu vya Kiswahili, magazeti, kamusi pamoja na kutumia miongozo mbalimbali. Hivi vyote hupelekea mtu kuweza kuongea Kiswahili kwa ufasaha.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili linahusiana na Sera ya Lugha…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa naomba ufupishe kidogo jibu linalofuata.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yetu inaendelea kukusanya maoni ya wadau kuhusiana na Sera ya Lugha ili kusudi kuweza kupata changamoto ambazo zinaikabili lugha yetu ya Kiswahili, lakini vile vile kujua ni jinsi gani tutazingatia masuala mbalimbali katika Sera ya Lugha na hivyo katika kipindi cha mwaka huu wa fedha 2016/2017 tunatarajia kwamba rasimu ya kwanza ya Sera ya Lugha itakuwa imekamilika na hivyo tuipeleke katika hatua za juu kwa ajili ya maamuzi.

Name

Mwantum Dau Haji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:- Matumizi yasiyo sahihi ya lugha ya Kiswahili kwenye vyombo vya habari hayatoi fursa ya kukua kwa lugha yetu na badala yake yanachangia kurithisha lugha yetu kwa watoto kwa namna iliyo mbovu; mathalani, Mtangazaji wa runiga au redio anasema “hichi” badala ya “hiki” au nyimbo hii badala ya “wimbo huu” na kadhalika. Je, Serikali ina mpango gani wa kimkakati wa kuvifanya vyombo vya habari kuwa mawakala wa kulinda usahihi wa lugha ya Kiswahili badala ya kuwa miongoni mwa wabomoaji wa lugha yetu?

Supplementary Question 2

MHE. MWANTUMU DAU HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na mimi kwa kuniona. Napenda kumuuliza Mheshimiwa Waziri wa Utamaduni, kuna baadhi ya nyimbo zinazoimbwa katika ma-stage show au zinazooneshwa katika runinga. Nyimbo hizi huwa zinatudhalilisha wanawake kuvaa yale mavazi yao ambayo yanaonesha, je, Serikali inazingatia suala hili au kisheria ni sawa kuimba nyimbo kama zile zinazotudhalilisha sisi wanawake?

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kuhusiana na nyimbo ambazo zinadhalilisha wanawake ni swali jipya naomba alilete vizuri ili kusudi tuweze kulijibu vizuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunavyo vyombo ambavyo vinasimamia kwa kupitia sheria zetu. Tuna Bodi ya Filamu ambayo huwa inaangalia, inapitia maudhui yenyewe kama ni ya filamu au wimbo, lakini pia tuna Kamati ya Maudhui ambayo ipo chini ya TCRA. Kwa hiyo, kwa kutumia sheria zetu tunadhibiti hali kama hii. Vilevile wale ambao wanaona kwamba hali hairidhishi, tunaomba wawasilishe ni wimbo upi au ni filamu ipi ili kusudi hatua stahiki ziweze kuchukuliwa.

Name

Ruth Hiyob Mollel

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:- Matumizi yasiyo sahihi ya lugha ya Kiswahili kwenye vyombo vya habari hayatoi fursa ya kukua kwa lugha yetu na badala yake yanachangia kurithisha lugha yetu kwa watoto kwa namna iliyo mbovu; mathalani, Mtangazaji wa runiga au redio anasema “hichi” badala ya “hiki” au nyimbo hii badala ya “wimbo huu” na kadhalika. Je, Serikali ina mpango gani wa kimkakati wa kuvifanya vyombo vya habari kuwa mawakala wa kulinda usahihi wa lugha ya Kiswahili badala ya kuwa miongoni mwa wabomoaji wa lugha yetu?

Supplementary Question 3

MHE. RUTH H. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ufasaha wa lugha yoyote ile ni ajira na Kiswahili ni kimojawapo. Tanzania ni kitovu cha lugha ya Kiswahili.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kufahamu Wizara ina mkakati gani wa kufunza na kutoa walimu wengi ambao wanaweza kupelekwa nchi mbalimbali, kwa mfano, Uganda, Rwanda sasa hivi wameanzisha Kiswahili kwenye shule zao na ninaamini Watanzania ndio wenye lugha fasaha ya Kiswahili. Je, kuna mkakati gani kufundisha walimu wa kutosha wa kuweza kuwapeleka nchi mbalimbali ambao wanazungumza Kiswahili na kutoa ajira kwa wananchi wetu? Ahsante.

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kweli kwamba kitovu cha Kiswahili ni hapa nchini kwetu Tanzania na kwa kulitambua hili, nchi za Afrika Mashariki wameamua Makao Makuu ya Kiswahili yawe hapa nchini na yamepelekwa Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo mafunzo ambayo yamekuwa yakitolewa na tumekuwa tukizalisha Walimu wa Kiswahili wengi kadri inavyowezekana; na siyo tu kuwazalisha, lakini kuwatafutia soko na wamekuwa wakipata masoko siyo tu katika Afrika na Afrika Mashariki, lakini hata nje ya nchi yetu na hasa China wamekuwa wakienda kwa wingi sana. Chuo Kikuu cha Zanzibar, kwa mfano SUZA, wamekuwa wakizalisha Walimu wengi sana wa Kiswahili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia huu mchakato sasa wa utengenezaji wa Sera ya Lugha ambao utaipa nguvu kubwa Kiswahili kama lugha ya nchi yetu, tutaweka mikakati ya kutosha ndani mle na sheria baada ya sera kukamilika ambayo itatusaidia zaidi kukifanya Kiswahili kiendelee kuwa bidhaa na hivyo kuwapa soko kubwa walimu ambao tutakuwa tukiwazalisha nchini kwetu.