Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza:- Bei za dawa za mifugo na kilimo zinaongezeka siku hadi siku na kufanya mfugaji mdogo ashindwe kupata maendeleo:- Je, Serikali ina utaratibu gani wa kudhibiti hali hiyo?

Supplementary Question 1

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali langu la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri ninalo swali la nyongeza.
Kwa kuwa wananchi wengi wa Mkoa wa Dar es salaam na hasa katika maeneo ya Kitunda, Mvuti, Chanika, Mbande, Pugu, Somangila, Kisarawe II, Kibada, Vijibweni, Yombo, Kunduchi, Mabwepande na Kibamba wote wanategemea kupata vipato vyao na hasa akina mama kwa kwa kazi ya kufuga kuku wa nyama na kuku wa mayai, lakini bei ya dawa zimekuwa kubwa sana kiasi kwamba akina mama hawa wanashindwa kuuza bidhaa zao, wanashindwa kuuza kuku wa mayai na kuku wa nyama kwa gharama ambayo ingeweza kuwapa faida.
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga maduka au kuweka dawa katika vituo vya mifugo vya Serikali ambavyo viko katika Wilaya zote Tanzania nzima ili wafugaji hawa waweze kupata nafuu ya bei za dawa kuliko vile wanavyolanguliwa na wafanyabiashara mbaimbali ambao wao hawana uchungu sana na wananchi, wao wanatafuta kipato?
Swali la pili, kwa kuwa Serikali imeonyesha wazi lengo lake kwamba kuna Kituo cha Tiba cha Kibaha kinaweza kuzalisha chanjo mbalimbali; je, Serikali ina mkakati gani wa kukiongezea nguvu kituo hiki ili iweze kuzalisha chanjo kwa wingi, wananchi waweze kupata chanjo hizo kwa bei nafuu na wao waweze kuboresha vipato vyao?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa kama alivyosema kwamba kuna changamoto kubwa sana ya upatikanaji wa dawa za mifugo, vilevile kwamba bei imekuwa ni bei ambayo wakulima wengi, wafugaji wengi hawawezi kustahimili. Mkakati wa Serikali kwa sasa ni kujaribu kuweka mazingira wezeshi kwa sekta binafsi ili iweze kutoa huduma hizo, huo ndiyo mwelekeo wa sera tuliyonayo ya mwaka 2006.
Hata hivyo, Serikali kwa kutambua kwamba tayari utaratibu huo una changamoto Serikali inafikiria zaidi kuangalia ni namna gani tunaweza tukawezesha na tukahamasisha ujenzi wa viwanda dawa hizo ziweze kuzalishwa nchini ili bei ipungue. Kwa sababu kinachofanya dawa kwa kiasi kikubwa ziwe ghali ni kwa sababu nyingi tunazitoa nje ya nchi, kwa hiyo kuna utaratibu ndiyo maana tunahamasisha sana kuhusu ujenzi wa viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ili kuteremsha na kufanya bei ya dawa hizo kuwa nafuu Serikali imeendelea kupitia wigo wa kodi na tozo mbalimbali ambazo ziko kwenye dawa ili hatimaye dawa hizo ziweze kupatikana kwa urahisi zaidi. Serikali inaendelea kutumia Maafisa Ugani kufanya uhamasishaji na kutoa elimu ili wananchi wenyewe waweze kuona umuhimu wa kutumia dawa ili kuweza kunusuru mifugo yao isife.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili kwamba Serikali ina mpango gani wa kuongezea kiwanda kilichopo Kibaha nguvu, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inaweka mazingira wezeshi ili sekta binafsi waweze kujenga viwanda zaidi. Kwa hiyo, tuko tayari kushirikiana na viwanda hivyo kwa sababu kuna viwanda vya Farmers Center, vilevile kuna kiwanda cha Multivet Services kwa hiyo zote hizi tutaendelea kufanya nao kazi na kutoa msaada ambao watahitaji ikiwa ni pamoja na msaada ambao watauhitaji ikiwa na nafuu za kodi ili waweze kuzalisha zaidi ili wakulima wetu na wafugaji wetu waweze kupata dawa kwa haraka lakini na kwa bei ambayo ni nzuri. (Makofi)