Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Tauhida Cassian Gallos Nyimbo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. TAUHIDA CASSIAN GALOSS aliuliza:- (a) Je, katika bajeti ya mwaka 2015/2016, Serikali imepeleka wanafunzi wangapi kusoma nje ya nchi? (b) Je, kada gani ambazo zilipewa kipaumbele?

Supplementary Question 1

MHE. TAUHIDA CASSIAN GALOSS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa suala la elimu ya juu ni suala la Muungano, je, wanafunzi wangapi katika idadi ya hao aliowataja wametokea Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, je, wanafunzi hawa wanaporudi masomoni hukuta ajira tayari au wanaachwa wanazurura mitaani?

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kimsingi nafasi hizi za kusoma nje mara nyingi zinapotolewa zinatangazwa kupitia Balozi husika ambazo zimepanga kutoa masomo hayo, lakini wakati mwingine pia kupitia vyuo vyetu vikuu. Wakati wa uombaji suala linalozingatiwa zaidi ni sifa ikizingatiwa kwamba masuala ya elimu ya juu ni masuala ya Muungano.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia wakati mwingine inawezekana kabisa Ubalozi ukaamua kama umependa watu wa Zanzibar, basi utaelekeza moja kwa moja kupitia masuala ya kimahusiano kwa upande wa Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kimsingi kwa sasa sitaweza kukupa taarifa kamili na ikizingatiwa kwamba linahitaji data. Kwa upande wa ajira, hawa wanafunzi wakirudi, kwa sababu wengi wanakuwa wamepelekwa kwa ajili ya jambo mahsusi, kwa mfano, upande wa gesi, kwa hiyo wanapofika yale maeneo ambayo yanawahitaji ndiyo ambayo yanakuwa yametangaza kazi na wakati huo huo wenye sifa wanakuwa wanachukuliwa kupitia taratibu zetu za kiutumishi.

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Primary Question

MHE. TAUHIDA CASSIAN GALOSS aliuliza:- (a) Je, katika bajeti ya mwaka 2015/2016, Serikali imepeleka wanafunzi wangapi kusoma nje ya nchi? (b) Je, kada gani ambazo zilipewa kipaumbele?

Supplementary Question 2

MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Suala la idadi ya wanafunzi ambao wametokana na bajeti linaendana na sifa za wanafunzi wanaotakiwa kujiunga na vyuo vikuu. Ningependa kuuliza swali dogo tu, kwamba, sasa hivi Serikali imetoa kauli mbili tofauti, mwezi Julai iliweka vigezo vya wanafunzi kujiunga na Chuo Kikuu vya GPA ya 3.5 kwa watu wa diploma, si zaidi ya hapo. Hata hivyo, juzi wametoa tena tamko lingine la GPA ya 3.0 kwa watu wa ordinary diploma. Je, Serikali itueleze hapa, ni kwa nini inawasumbua wanafunzi katika kipindi hiki ambacho wanafunzi wengi walikuwa wameshakata tamaa na hawaku-apply katika Vyuo Vikuu? Ahsante.

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, kama ambavyo siku Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania analihutubia Bunge; alisisitiza kwamba Awamu hii ya Tano, jukumu lake kubwa litakuwa ni kuongeza ubora. Vile vile lazima ikumbukwe kwamba, Serikali kwa kushirikiana na wananchi imefanya kazi kubwa ya kuwezesha wanafunzi wengi kusoma na kiasi kwamba tunao wengi wenye sifa za ufaulu wa juu. Hiyo imejidhihirisha wazi hata katika udahili wa mwaka huu wa Vyuo Vikuu, waombaji ni wengi na waliofaulu ni wengi sana kiasi cha kupandisha zile points ili tuweze kuendana na haki katika kuwachukua.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika suala hilo katika maeneo hayo pia kuna ushindani mkubwa, lakini Wizara kila wakati inaangalia kama hao watu wenye sifa hizo itaonekana kwamba hawapatikani hapo ndipo tunaweza tukafikiria zaidi namna ya kusema tushuke chini, lakini kama wanapatikana basi hamna haja ya kumchukua mtu ambaye ana ufaulu wa chini ukamuacha mtu ambaye ana ufaulu wa kiwango cha juu.