Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Cosato David Chumi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafinga Mjini

Primary Question

MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:- Sudan Kusini imekubaliwa kujiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki. Je, ni lini Serikali itafungua Ubalozi katika nchi hiyo ili kutengeneza mazingira ya kunufaika na fursa zilizoko katika nchi hiyo?

Supplementary Question 1

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu imeeleza kwamba kufunguliwa kwa Ubalozi kutategemea masuala ya kibajeti; je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kufungua ile tunaita Honorary Consul kwa sababu ile haina gharama zozote ambazo Serikali itaingia zaidi ya kupata tu mtu ambaye ni mwaminifu na mwadilifu?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kufungua Honorary Consuel ambapo siyo suala lenye gharama kibajeti kama ambavyo Serikali imejibu katika swali la msingi, ni jambo la msingi kwa sababu litawezesha kufungua fursa zaidi za kiuwekezaji siyo tu katika Sudan ya Kusini, lakini pia katika maeneo mengine ambako Serikali imeshindwa kufungua Balozi kwa sababu ya ukosefu wa fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa kufungua fursa hizi za uwakilishi wa heshima, tunapanua wigo wa kuongeza uwekezaji na biashara na hivyo kuongeza mapato ya Serikali ambayo mwisho wa siku wananchi wa Mafinga na Tanzania kwa ujumla watanufaika katika kuboresha huduma zao za kijamii. (Makofi)
Je, Serikali iko tayari pia sasa kufungua Uwakilishi wa Heshima katika Mji wa Lubumbashi ambako kuna fursa kubwa za kibiashara baina yetu sisi Tanzania na nchi ya Demokrasia ya Kongo? (Makofi)

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli alivyosema Mheshimiwa Mbunge kwamba kufungua Uwakilishi wa Heshima ni njia mojawapo ya kuwa na uwakilishi wa nchi yetu katika nchi nyingine, lakini vilevile kuna utaratibu wa Kikonseli lakini na ule utaratibu wa kawaida wa kufungua Ubalozi wenyewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, hizo ni kati ya njia ambazo tungeweza kutumia nchini Sudan Kusini, lakini kwa sasa Wizara inafikiria zaidi kujipanga kufungua Ubalozi kamili badala ya kufungua Consul au kutafuta Uwakilishi wa Heshima. Hii ni kwa sababu nchi ya Sudan Kusini ni moja kati ya wanachama wa Jumuya yetu ya Afrika Mashariki, kwa hiyo, ningependa kuwa na Ubalozi kamili.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wakati bado tunaelekea kule, tunajipanga, nimfahamishe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kitendo cha nchi ya Sudan Kusini kujiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki inatoa fursa nyingi sana na inarahisisha wananchi kuweza kunufaika na fursa zilizoko kule hata bila kuwepo na Ubalozi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki unaruhusu pamoja na mambo mengine urahisi wa kusafirisha bidhaa, lakini vilevile huduma na kazi kwenye hizi ambazo ni wanachama.
Kwa hiyo, tayari kuna mazingira mazuri ambayo yanarahisisha wananchi kuweza kunufaika na hizo fursa hata bila kuwa na uwakilishi wa kiheshima bila kuwa na Consul au kuwa na Ubalozi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema Wizara inajipanga, tunatambua umuhimu wa Sudan Kusini kama wanachama wa Afrika ya Mashariki, tunatambua fursa lakini huko ndiyo tunaelekea, lakini tunajipanga.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Mheshimiwa Mbunge amezungumzia kuhusu kufungua Uwakilishi wa Kiheshima Lubumbashi. Napenda kumjibu Mheshimiwa Mbunge kwamba, ni kweli kabisa tunatambua fursa zilizopo Lubumbashi, tunafahamu fursa zilizopo katika ukanda huo wa DRC, lakini kwa sasa Serikali na Wizara imejielekeza zaidi katika kuimarisha shughuli za Kibalozi kwa sababu tunafikiri bado inakidhi matakwa hayo ya fursa zilizopo, nashukuru sana.