Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Name
Abdulaziz Mohamed Abood
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Morogoro Mjini
Primary Question
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD aliuliza:- Morogoro Mjini bado ina kero ya maji katika maeneo mbalimbali ya Manispaa kama vile Kata ya Tungi, Mkundi, Kiegea A na B, Kihonda, Kisanga na Ngerengere:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuondoa kero hii ya maji katika Manispaa ya Morogoro?
Supplementary Question 1
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD: Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili mafupi ya nyongeza. Kwa kuwa Serikali ina mpango wa kusambaza mabomba maeneo ambayo hayana mabomba ya maji, nataka kujua muda gani ambao Serikali itasambaza mabomba hayo?
Swali la pili, kuna baadhi ya maeneo Morogoro Mjini hawapati maji karibu miezi miwili, lakini cha kushangaza wanapelekewa bili za kulipa maji, je, ni lini Serikali itaondoa kero hiyo ambayo imekuwa kama dhuluma kwa wananchi wa Jimbo la Morogoro Mjini?
Name
Eng. Isack Aloyce Kamwelwe
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Katavi
Answer
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ni muda gani tutakamilisha kuweka mtandao wa mabomba ya kusambaza maji ili yaweze kufika maeneo yote.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge Abood aangalie katika kitabu cha bajeti, tumetenga zaidi ya shilingi bilioni nne kwa mwaka wa fedha unaokuja wa 2016/2017 kwa ajili ya kuendelea na kazi ya kuweka mabomba ya mtandao katika Jimbo lake la Morogoro Mjini. Kwa hiyo ni muda gani, kwa sababu utekelezaji una mchakato wake, mchakato wa bajeti tayari umekamilika fedha Serikali imetenga. Kwa hiyo, tutaendelea na usanifu, tutaendelea na kutangaza tenda na baada ya kutangaza tenda kumpata mkandarasi ndiyo program kamili lini tutatekeleza mradi kwa miezi mingapi itapatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu tatizo la bili za maji. Nashukuru kwamba nimepata hii taarifa, Mheshimiwa Mbunge hili suala tutalifuatilia kuona inakuwaje kwamba mtu analetewa bili za maji wakati maji hatumii?
Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili nililikuta pia katika Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara nilipokwenda kule. Suala hili wakati mwingine linakuwa na udanganyifu. Kuna connection ambazo hazijatambuliwa na mamlaka, mtu anaiba maji, sasa wakimtambua wanakwenda kumpiga bili analalamika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mambo mengi ambayo yanajitokeza katika hili suala la bili, lakini pia kuna uzembe vile vile hata ndani ya watendaji wetu kwa upande wa mamlaka. Kwa hiyo, nimwombe tu Mheshimiwa Abood tushirikiane. Nitatoa taarifa kwa Mamlaka ya Mji wa Morogoro ili waweze kuliangalia hili na tutampatia majibu.
Name
Flatei Gregory Massay
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Mbulu Vijijini
Primary Question
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD aliuliza:- Morogoro Mjini bado ina kero ya maji katika maeneo mbalimbali ya Manispaa kama vile Kata ya Tungi, Mkundi, Kiegea A na B, Kihonda, Kisanga na Ngerengere:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuondoa kero hii ya maji katika Manispaa ya Morogoro?
Supplementary Question 2
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Jimbo la Morogoro Mjini linafanana kabisa na Jimbo la Mbulu Vijijini juu ya tatizo hili la ukosefu wa maji. Kwa kuwa Waziri alishaniahidi kwamba tukipeleka certificate atawasaidia wakandarasi kuwalipa fedha waendelee na mradi. Je, ni lini sasa watapatiwa fedha, miradi ya Mbulu iliyopo Haidom na Dongobeshi ili wakandarasi waweze kumalizia na wananchi wapate maji? Ahsante
Name
Eng. Isack Aloyce Kamwelwe
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Katavi
Answer
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru. Tumekuwa na matatizo huko nyuma kwamba, tunapeleka fedha katika Halmashauri wanachelewa kutekeleza miradi. Sasa hivi tumeweka utaratibu kwamba tukishatenga bajeti, basi Halmashauri zitangaze tenda zianze kutekeleza miradi. Certificate ikipatikana watuletee tutaipeleka Hazina, halafu wakitupatia pesa ndiyo tuweze kupeleka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama tulivyoongea kama ulivyosema Mheshimiwa Massay naendelea kusisitiza kwamba walete certificate halafu pesa tutalipa.
Name
Mohamed Omary Mchengerwa
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Rufiji
Primary Question
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD aliuliza:- Morogoro Mjini bado ina kero ya maji katika maeneo mbalimbali ya Manispaa kama vile Kata ya Tungi, Mkundi, Kiegea A na B, Kihonda, Kisanga na Ngerengere:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuondoa kero hii ya maji katika Manispaa ya Morogoro?
Supplementary Question 3
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Naibu Spika, matatizo ya maji katika Jimbo langu la Rufiji ni makubwa na hatuwezi kuyafananisha na Morogoro. Eneo dogo la Rufiji ambalo linapata maji safi ni Tarafa ya Ikwiriri, lakini tumeharibikiwa motor pump huu sasa mwezi wa Nane. Tuliwasilisha maombi kwa Mheshimiwa Waziri lakini mpaka leo hii hatujapata motor pump hiyo au kupata fedha kwa ajili ya ununuzi wa motor pump ili kuweza kuwasaidia wananchi wa Jimbo langu la Rufiji.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nipate taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, ni lini sasa fedha hizi zitatoka kwa ajili ya ununuzi wa motor pump ili kuweza kuwasaidia wananchi wa Jimbo langu la Rufiji hususan Tarafa ya Ikwiriri? Ahsante.
Name
Eng. Gerson Hosea Lwenge
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Wanging'ombe
Answer
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa ni mwezi wa Sita na mmepitisha bajeti ya Wizara ya Maji ambayo utekelezaji wa bajeti unaanza Julai. Sasa naomba tusubiri fedha za Mwaka wa Fedha wa 2016/2017 itakapotoka ndipo tuweze kumpatia Mheshimiwa Mbunge.
Name
Yahaya Omary Massare
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Manyoni Magharibi
Primary Question
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD aliuliza:- Morogoro Mjini bado ina kero ya maji katika maeneo mbalimbali ya Manispaa kama vile Kata ya Tungi, Mkundi, Kiegea A na B, Kihonda, Kisanga na Ngerengere:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuondoa kero hii ya maji katika Manispaa ya Morogoro?
Supplementary Question 4
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona ili niulize swali dogo tu la nyongeza, kwa kuwa swali la msingi wananchi wa Morogoro linafanana sana na wananchi wa Jimbo la Manyoni Magharibi hususan Mji mdogo wa Itigi. Je, ni lini Serikali itasaidiana na Halmashauri yangu kuhakikisha Vijiji vya Rungwa, Kintanula, Kalangali, Mitundu, Kingwi, Dodiandole, Mbugani, Mabondeni, Njirii, Gurungu, Majengo, Songambele, Kitalaka, Kihanju na Tambuka Reli vitapatiwa maji? Ahsante.
Name
Eng. Isack Aloyce Kamwelwe
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Katavi
Answer
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kushirikiana na Halmashauri zote nchini kwa kuzipangia bajeti ili ziweze kutekeleza miradi ya maji. Hilo limeshafanyika, katika Mwaka wa Fedha unaokuja Serikali imehakikisha Halmashauri zote inazipatia fedha kwa ajili ya kuendeleza miradi ya maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha zilizotolewa kwanza ni kuhakikisha kwamba miradi iliyokuwa inaendelea inakamilika, baada ya hapo ndipo wanakwenda sasa kwenye miradi mipya. Kwa hiyo, kwa mujibu wa swali lake Serikali tayari inashirikiana na Halmashauri, sasa ni wajibu wake Mheshimiwa Mbunge, kwa sababu na yeye ni Diwani, kukaa katika kikao cha Madiwani na uongozi wa Halmashauri ili waweze kupanga bajeti kwa hela iliyotengwa ili hivyo vijiji viweze kufikiwa. Kama fedha haitatosha basi mwaka ujao wa fedha wataleta maombi, tutatenga fedha nyingine.