Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 45 Energy and Minerals Wizara ya Nishat 386 2016-06-17

Name

Dr. Raphael Masunga Chegeni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busega

Primary Question

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI aliuliza:-
Mradi wa REA II ulitarajia kuvipatia umeme vijiji vyote vya Jimbo la Busega na kumekuwepo na kusuasua kwa utekelezaji wa mradi huo jimboni humo:-
(a) Je, mpaka sasa ni vijiji vingapi vimepatiwa umeme kupitia mradi huo?
(b) Je, ni lini vijiji vilivyobaki vitapatiwa umeme?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Raphael Masunga Chegeni, Mbunge wa Busega, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya vijiji 13 vimepatiwa umeme katika Jimbo la Busega kupitia mradi kabambe wa REA Awamu ya II unaoendelea kutekelezwa hivi sasa. Mradi huu utakamilika mwishoni mwa mwezi Juni, 2016 ambapo vijiji vyote 18 vitapatiwa umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme Wilaya ya Busega inayotekelezwa na Mkandarasi Sengerema Engineering Group inajumuisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 91.6; ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 52; ufungaji wa transfoma 33 za ukubwa mbalimbali pamoja na kuwaunganishia umeme wateja 932.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi umekamilika kwa asilimia 94 ambapo ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 umekamilika kwa asilimia 97; ujenzi wa njia ya msongo wa kilovoti 0.4 umekamilika kwa asilimia 93 na transfoma 18 zimefungwa. Wateja 420 wameunganishiwa umeme. Kazi hii itagharimu jumla ya shilingi bilioni 4.88.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji ambavyo havikujumuishwa katika mradi kabambe wa REA Awamu ya II vitapatiwa umeme katika Mradi wa REA Awamu ya III utakaoanza mwezi Julai, 2016. Kazi ya kupeleka umeme katika maeneo hayo itajumuisha ujenzi wa njia ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 68; ujenzi wa njia ya umeme ya kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 198; na ufungaji wa transfoma 19 za ukubwa mbalimbali. Pamoja na kazi hizo pia wateja 6,096 wataunganishiwa umeme. Kazi hii itagharimu shilingi bilioni 8.6.