Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 28 Energy and Minerals Wizara ya Nishat 247 2022-05-23

Name

George Natany Malima

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Primary Question

MHE. GEORGE N. MALIMA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo la kukatika kwa umeme katika Mji wa Mpwapwa?

Name

Stephen Lujwahuka Byabato

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa George Natany Malima, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, awali Mji wa Mpwapwa pamoja na maeneo ya Wilaya za Mpwapwa, Kibaigwa na Kongwa zilikuwa zinapata huduma ya umeme kupitia njia ya ya umeme ya Mpunguzi yenye msongo wa kilovoti 33 na urefu wa kilometa 660.4 kutoka katika kituo cha kupoza umeme cha Zuzu, Dodoma Mjini. Kutokana na urefu na uchakavu wa njia hiyo, kulikuwepo na tatizo la kupungua kwa nguvu za umeme yaani low voltage katika maeneo ya Wilaya za Kongwa na Mpwapwa. Hata hivyo, Serikali kupitia TANESCO ilikamilisha ufungaji wa kifaa kiitwacho AVR yaani Automatic Voltage Regulator katika eneo la Kibaigwa na hivyo kufanikiwa kupunguza tatizo hilo.

Mheshimiwa Spika, tarehe 3 Agosti, 2021 Serikali kupitia TANESCO ilikamilisha ujenzi wa njia mpya ya kusambaza umeme ya msongo wa kilovoti 33 inayohudumia maeneo ya Wilaya za Kongwa na Mpwapwa. Kukamilika kwa ujenzi wa njia hii kumefanya njia iliyokuwepo awali kuendelea kuhudumia maeneo ya Kibaigwa pekee na hivyo kufanya maeneo ya Kongwa na Mpwapwa kuwa na umeme wa kutosha.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO inaendelea kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme nchini ikiwemo Wilaya ya Mpwapwa na katika mwaka wa fedha 2022/2023 TANESCO itatengewa shilingi bilioni 2.3 kwa ajili ya kufanya matengenezo na kuboresha nguvu za umeme katika njia chepushi za umeme yaani spur lines ikiwa ni pamoja na kubadilisha nguzo za miti kuweka za zege hasa katika maeneo korofi, kubadilisha vikombe na nyaya zilizochakaa pamoja na kufunga vikata umeme vinavyojiendesha vyenyewe yaani auto reclosers. (Makofi)