Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 28 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 238 2022-05-23

Name

Silvestry Fransis Koka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Mjini

Primary Question

MHE. SYLVESTRY F. KOKA aliuliza:-

Je, ni lini Mji wa Kibaha utakuwa Manispaa ambao kwa sasa ni Makao Makuu ya Mkoa wa Pwani?

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sylvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Halmashauri huanzishwa au kupandishwa hadhi kwa mujibu wa Sheria za Serikali za Mitaa Sura ya 287 na 288 pamoja na Mwongozo wa Uanzishwaji wa Maeneo ya Utawala wa mwaka 2014 ambao umeainisha vigezo na taratibu zinazopaswa kufuatwa ili kuanzisha au kupandisha hadhi Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, ni kweli mapendekezo ya kupandisha hadhi Halmashauri ya Mji Kibaha kuwa Manispaa yaliwasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Mapendekezo hayo yalifanyiwa uhakiki na timu ya wataalam kutoka Ofisi ya Rais-TAMISEMI mwaka 2016 kati ya vigezo 20 Halmashauri ya Mji wa Kibaha ilikuwa imekidhi vigezo 15 sawa na asilimia 75 tu.

Mheshimiwa Spika, vigezo ambavyo havikuwa vimefikiwa na Mji wa Kibaha ni pamoja na idadi ya watu, idadi ya kata na mitaa, kutokuwa na mpango kabambe wa uendelezaji mji, kutofikia asilimia zinazohitajika za wakazi waliokuwa wameunganishwa na huduma ya maji. Hivyo, Halmashauri hii haikuweza kupandishwa hadhi kwa kuwa ililazimu kukidhi vigezo vyote kwa pamaoja kwa mujibu wa Mwongozo wa Kuanzisha Maeneo ya Utawala wa mwaka 2014 ili kupandishwa hadhi ya kuwa Halmashauri ya Manispaa.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hizo za Halmashauri ya Mji wa Kibaha, Serikali kwa sasa inakusudia kuimarisha maeneo yaliyopo ili yaweze kutoa huduma zilizokusudiwa ikiwa ni pamoja na miradi ya maendeleo. Hivyo, ninashauri Halmashauri ya Kibaha, kujikita katika kuboresha zaidi huduma za wananchi.