Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 3 Foreign Affairs and International Cooperation Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 34 2016-09-08

Name

Munde Abdallah Tambwe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MUNDE T. ABDALLAH aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango mkakati gani kupitia diplomasia ya uchumi na nchi ya China kuunganisha wajasiriamali wadogo, wa kati na wakubwa ili kuingia ubia wa kuimarisha viwanda vidogo na vya kati?

Name

Dr. Susan Alphonce Kolimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Munde Abdallah Tambwe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kwamba nchi yetu ni miongoni mwa nchi nne Barani Afrika ambazo Serikali ya China imezichagua kuwekeza viwanda vyake katika miaka mitatu ijayo (2016 mpaka 2018). Kufuatia uamuzi huo Majimbo mawili ya China ya Jiangsu na Zhejiang yamekwishaelekezwa kuwekeza nchini.
Mheshimiwa Spika, Serikali ya China imeanzisha Mfuko Maalum wa Fedha kwa ajili ya kuwezesha wafanyabiashara wadogo na wa kati wa Afrika kupata mitaji maalum. Mfuko huo umewekwa katika Benki ya Maendeleo ya China na tayari umetengewa dola za Kimarekani bilioni tano. Serikali imekwishaanza mazungumzo na benki hiyo kwa ajili ya kuwezesha mabenki nchini yaweze kukopa fedha hizo ili hatimaye yaweze kuwakopesha wajasiriamali wetu wanaotaka kuwekeza kwenye sekta ya viwanda kwa kushirikiana na wenzao wa China.
Mheshimiwa Spika, tarehe 22 Agosti, 2016 Wizara yangu iliitisha kikao cha pamoja kati ya Benki ya Maendeleo ya China na mabenki ya Tanzania ili kupewa utaratibu wa namna ya kupata fedha za mfuko huo. Matarajio yetu ni kwamba, mabenki hayo yatakidhi vigezo vya kuchukua fedha kutoka katika Mfuko huo wa China, ili Watanzania waanze kupata mitaji mapema iwezekanavyo.
Mheshimiwa Spika, ubalozi wetu nchini China mara kwa mara umekuwa ukiwashawishi wafanyabiashara wa China waje kuwekeza nchini na mara kadhaa umeandaa ziara za makampuni mbalimbali ya China kuja nchini kuonana na Kituo chetu cha Uwekezaji (TIC).
Mheshimiwa Spika, kwa taarifa zilizopo TIC wameendelea kutekeleza wajibu wao kwa ufanisi mkubwa ambao makampuni mbalimbali ya China yameingia ubia na Watanzania kuanzisha viwanda nchini. Mfano mzuri ni ujenzi wa kiwanda kikubwa cha kuzalisha nondo na bidhaa za chuma kinachojengwa Kibaha, Mkoani Pwani kwa ubia kati ya Watanzania na Wachina. Kiwanda hicho kitakapokamilika kitazalisha ajira nyingi kwa ajili ya vijana wa Kitanzania.