Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 37 Public Service Management Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 483 2023-05-31

Name

Sophia Hebron Mwakagenda

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA aliuliza:-

Je, kwa nini Serikali inaajiri kwa kigezo cha mwaka wa kumaliza chuo na kupitia mafunzo ya jeshi?

Name

Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kutoa ajira kwa kada mbalimbali zinazohitajika katika Utumishi wa Umma, Serikali imekuwa ikizingatia Sera ya Menejimenti ya Ajira na Utumishi wa Umma Toleo la 2 la mwaka 2008 aya ya 4.2 ambayo inataka zoezi la ajira katika Utumishi wa Umma liendeshwe kwa wazi na ushindani ili kuwezesha Serikali kupata watumishi wenye utaalam na sifa stahiki kwa kuzingatia uwezo, weledi na umahiri wa waombaji fursa za ajira.

Mheshimiwa Spika, ili kuleta ushindani katika soko la ajira, vigezo mbalimbali hutumika kuzingatia mazingira maalum au mazingira mahsusi ya waajiri. Katika vyombo vya Ulinzi na Usalama na Taasisi zilizoingia katika mfumo wa Jeshi USU kutokana masharti ya kazi hizo na mahitaji maalum au mahsusi ya vyombo husika, ajira zinazotolewa kwa kigezo cha ukomo wa umri na kigezo cha kupitia Mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa.

Mheshimiwa Spika, kada nyingine katika Taasisi za Umma nje ya Vyombo vya Ulinzi na Usalama na Taasisi zenye mfumo wa Jeshi USU kigezo cha Kupitia Mafunzo ya Jeshi hakitumiki. Hata hivyo, waombaji wa fursa za Ajira Serikalini kwa masharti ya kudumu Serikali wanatakiwa kuzingatia Kanuni ya D. 39 ya Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009 ambayo inawataka wasiwe na umri usiopungua miaka 18 na wasiozidi umri wa miaka 45 kwa lengo la kuwawezesha kuchangia katika Mifuko ya Hifadhi ya Jamii walau kwa miaka 15 ili kustahili kulipwa pensheni.