Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 2 Good Governance Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 18 2023-04-05

Name

Zahor Mohamed Haji

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwera

Primary Question

MHE. ZAHOR MOHAMMED HAJI aliuliza: -

Je, Serikali inachukua hatua gani kwa viongozi wanaowanyima wananchi kwa makusudi haki yao ya kuwa wanufaika wa TASAF?

Name

Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kabla sijajibu swali namba 18 lililoulizwa na Mheshimiwa Zahor Mohammed Haji naomba kutumia nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuniamini. Nataka nimwakikishie yeye na watanzania wote kwamba tutaendelea kufanya kazi na kazi itaendelea.

Mheshimiwa Spika, Sasa, kwa niaba ya Waziri wa Nchi ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na utawala Bora, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zahor Mohammed Haji Mbunge wa Mwera kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, zoezi la utambuzi wa wanufaika wa TASAF ni zoezi shirikishi na hujumuisha Wataalam kutoka Halmashauri, Maafisa wa TASAF, Wananchi wa maeneo husika yanayosimamiwa na viongozi wa vijiji/mitaa/shehia.

Mheshimiwa Spika, inapotokea kiongozi au viongozi wamewanyima haki wananchi kwa makusudi bila sababu yoyote ile hatua zifuatazo huchukuliwa dhidi yao: -

(a) Endapo uongozi wa vijiji/mitaa/shehia utashinikiza kuondoa majina ya kaya kwenye orodha ya utambuzi bila kuafikiwa na jamii, zoezi la utambuzi husitishwa na taarifa hupelekwa kwa Mkurugenzi wa Halmashauri/Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais (Zanzibar) na nakala hupelekwa kwa Mkurugenzi wa TASAF.

(b) Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri/Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais (Zanzibar) huchunguza tuhuma hizo na ikithibitisha tuhuma hizo mhusika husitishwa kujihusisha na shughuli zozote za Mpango wa TASAF. Aidha, baada ya kusimamishwa, mhusika huchukuliwa hatua za kinidhamu ikiwa ni pamoja na kupewa karipio au kuondolewa kwenye nafasi yake.