Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 32 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Maliasili na Utalii 259 2016-05-30

Name

Josephine Johnson Genzabuke

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

Pori la Akiba la Kagera Nkanda lililopo Wilaya ya Kasulu lilianzishwa kipindi ambacho Wilaya ya Kasulu ilikuwa na wakazi wachache na kwa sasa idadi ya watu katika Wilaya hiyo imekuwa kubwa na kufanya mahitaji ya ardhi kuwa makubwa, pia hivyo kusababisha mgogoro baina ya wakulima na wafugaji na mamlaka za misitu na wanyaa pori.
Je, Serikali imejipanga vipi kumaliza migogoro hii na kuwasaidia wananchi?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Augustine Vuma Holle, Mbunge wa Kasulu Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Kagera Nkanda ni kijiji kilichopakana na Hifadhi ya Msitu wa Makere Kusini na si Pori la Akiba. Msitu huu ulihifadhiwa kwa Tangazo la Serikali Namba 250 la mwaka 1956 na una ukubwa wa hekta 99,682.7. Uhifadhi wa msitu huo unatokana na umuhimu na faida zake kwa Taifa ikiwa ni pamoja na kuwa chanzo kikuu cha maji yanayoingia kwenye Mto Malagarasi, ushoroba wa wanyamapori kati ya Pori la Akiba Moyowosi na Kigosi, sehemu ya eneo la ardhi oevu lenye umuhimu wa kimataifa (The Malagarasi Moyowosi Ramsar Site), Hifadhi ya viumbe na mimea na hivyo kusaidia kupunguza madhara ya mabadiliko ya tabianchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, chanzo cha migogoro na wananchi wanaoishi jirani na hifadhi hii ni mahitaji ya ardhi kwa ajili ya shughuli za kibinadamu hususani kilimo. Swali hili limejibiwa na Serikali mara mbili ndani ya Bunge lako Tukufu, ambapo mara moja lilijibiwa na Wizara ya Maliasili na Utalii tarehe 26 Juni, 2014 na mara nyingine lilijibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI mnamo tarehe 18 Juni, 2015.
Mheshimiwa Naibu Spika, viongozi mbalimbali akiwemo Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Awamu ya Nne walifanya ziara katika eneo husika na kusikiliza hoja kutoka kwa wananchi, lakini kumbukumbu zinaonesha kuwa hakuna madai yaliyotolewa kuhusiana na uhitaji wa ardhi ya hifadhi kutoka kwa wananchi ispokuwa kwamba baadhi ya wananchi walivamia msitu wamekuwa wakiomba na kuruhusiwa kuvuna mazao waliyoyapanda kabla Serikali haijatekeleza operesheni ya kuwaondoa katika hifadhi ya msitu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu haya, wakati wa zoezi la kushughulikia matatizo ya ardhi kwa nchi nzima ikihusisha Wizara sita, zoezi ambalo litaanza baada ya Bunge la Bajeti, Wizara yangu itazingatia wito uliotolewa Bungeni kupitia jibu la msingi lililotolewa na TAMISEMI mnamo tarehe 18 Juni, 2015 kuhusu mgogoro huu.