Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 47 Youth, Disabled, Labor and Employment Ofisi ya Rais TAMISEMI. 399 2016-06-21

Name

Salome Wycliffe Makamba

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI (K.n.y MHE. SALOME W. MAKAMBA) aliuliza:-
Wafanyakazi wa migodi ya uchimbaji wa madini hufukuzwa kazi kiholela bila kulipwa fidia stahiki kutokana na ulemavu na magonjwa yanayosababishwa na vitendea kazi hatarishi wakati wakiwa kazini.
(a) Je, Serikali iko tayari kuzuia kuingizwa nchini vitendea kazi hatarishi na kufunga migodi ambayo ina wahanga wengi na ulemavu na magonjwa yatokanayo na shughuli za uchimbaji madini?
(b) Je, ni lini Serikali itaanza kutumia Sheria ya Fidia Na. 20 ya mwaka 2008 ili wafanyakazi wa migodini walipwe fidia stahiki wanapopata ulemavu au magonjwa wanapokuwa kazini badala ya Sheria ya Fidia ya mwaka 2002? na
(c) Je, Serikali inatoa tamko gani kwa waajiri wanaowatelekeza wafanyakazi waliopata ulemavu wakiwa kazini na kukataa kuendelea kulipa gharama za matibabu yao?

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri Mkuu naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salome Makamba, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia taasisi zake na sheria mbalimbali za nchi inao utaratibu madhubuti wa kudhibiti uingizwaji wa bidhaa zisizo na ubora pamoja na vitendea kazi hatarishi kwa afya za wafanyakazi mahali pa kazi ikiwemo migodini.
Aidha, Sheria ya Afya na Usalama Mahali pa Kazi ya mwaka 2003, imeipa mamlaka Wakala wa Afya na Usalama Mahali pa Kazi kukagua vitendea kazi vinavyotumika mahali pa kazi ikiwa ni pamoja na migodi na kupima afya za wafanyakazi.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi Namba 20 ya mwaka 2008 ilitungwa ili kulipa fidia kwa wafanyakazi wanaoumia au kupata madhara au kufariki wakiwa kazini, ikiwa ni pamoja na wafanyakazi wa migodini wanaopata ajali.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria namba 20 itaanza kutoa rasmi fidia kwa wafanyakazi tarehe 1/7/2016. Kipindi hiki waajiri wote waendelee kutumia Sheria Na. 263 kuhakikisha wafanyakazi wanahudumiwa na kulipwa wawapo kazini. Aidha, Serikali inatoa onyo kwa waajiri ambao hawataki kutenda haki ya kuwalipa fidia kwa mujibu wa sheria.