Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 9 Energy and Minerals Wizara ya Madini 77 2022-04-20

Name

Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Primary Question

MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza: -

Je, Serikali ina taarifa gani juu ya Madini yanayopatikana Wilaya ya Urambo na lini itawasaidia Wananchi ili wanufaike na Madini hayo?

Name

Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Jimbo la Urambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa tafiti zilizowahi kufanywa na GST kuhusu madini yapatikanayo nchini, Wilaya ya Urambo ina madini mbalimbali lakini ni kidogo sana. Madini hayo ni kama vile dhahabu, urani, shaba, malbo, udongo mfinyanzi au clay na miamba migumu ya ujenzi mfano granite. Pamoja na Wilaya hiyo kuwa na kiwango kidogo cha madini kwa tafiti zilizokwishafanyika, zipo leseni Nne (04) za uchimbaji mdogo. Lakini katika leseni hizo, leseni Tatu (03) ni za uchimbaji mdogo wa madini ujenzi na leseni Moja (01) ni ya uchimbaji mdogo wa madini ya dhahabu.

Mheshimiwa Spika, GST ambayo ni taasisi yetu ya Jiolojia (Geological Survey of Tanzania) inaendelea kuhuisha kitabu chake cha madini yapatikanayo katika Mikoa yote Tanzania Bara na kwa sasa tayari Mkoa wa Tabora na Wilaya zake ikiwemo Wilaya ya Urambo ni moja kati ya mikoa itakayofanyiwa utafiti kwa lengo la kuhuisha kitabu hicho.

Mheshimiwa Spika, mara baada ya utafiti huo kukamilika, ramani ya uwepo wa madini hadi ngazi ya kijiji itaandaliwa na wananchi kupata taarifa hizo kupitia Serikali ya Kijiji na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya. Taarifa hizo zitawasaidia wananchi wote ikiwa ni pamoja na wananchi wa Wilaya ya Urambo kuwekeza katika sekta ya Madini kwa ujumla.