Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 10 Sitting 6 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 102 2023-02-07

Name

Ritta Enespher Kabati

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. RITTA E. KABATI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali italeta sheria ya wamiliki wa vyombo vya usafiri kuwa na miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu?

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Answer

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dokta Ritta Kabati, Mbunge wa viti maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2019, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilipitisha Sheria ya kuanzishwa kwa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) na kuweka kifungu katika Sheria hiyo kinachozingatia uwepo wa miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kifungu cha 6(e) cha Sheria ya Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini Sura ya 413, kimeeleza kuwa moja ya Majukumu ya LATRA ni kuhakikisha uwepo wa huduma ya usafiri wa umma unaoweza kutumiwa na watu wote wakiwemo watu wenye vipato vya chini, waishio vijijini, na watu wenye mahitaji maalum ambayo inajumuisha watu wenye ulemavu. Aidha, Kifungu cha 5(c) (i) na (ii) kimeeleza kuwa moja ya Kazi za LATRA ni kuweka viwango vya bidhaa na huduma pamoja na vigezo na masharti ya utoaji wa huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, itakumbukwa kuwa kupitia marekebisho ya Sheria ya Fedha ya mwaka 2022, Kifungu cha 5(1) na (2) cha Sheria ya Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini Sura ya 415 kilirekebishwa kwa kuiondolea LATRA jukumu la kuweka viwango vya bidhaa na huduma zinazodhibitiwa. Jukumu hilo kwa sasa linatekelezwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) ambalo ndilo lenye dhamana ya kuweka viwango vya bidhaa na huduma mbalimbali nchini. LATRA imebaki na jukumu la kusimamia utekelezaji wa viwango na kuweka masharti na vigezo vya bidhaa na huduma zinazodhibitiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naielekeza LATRA ishirikiane na TBS katika kuweka na kusimamia utekelezaji wa viwango vya vyombo vya usafiri wa umma ili viwe na miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu. Ahsante.