Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 26 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 211 2016-05-23

Name

Devotha Methew Minja

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. MHE. DEVOTHA M. MINJA) aliuliza:-
Askari wa Jeshi la Polisi na Magereza wanaishi katika nyumba chakavu zisizokuwa na hadhi ukilinganisha na kazi zao wanazofanya kwa jamii.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwaboreshea makazi.

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Mathew Minja, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama yalivyowahi kujibiwa maswali kama haya ndani ya Bunge lako Tukufu mara kadhaa kuhusu Askari kuboreshewa makazi yao, Serikali inafahamu kuwa lipo tatizo la baadhi ya Askari wa Jeshi la Magereza na Polisi kuishi katika nyumba chakavu zisizokuwa na hadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na tatizo hili Serikali imeendelea na mpango wa kuzifanyia ukarabati mkubwa baadhi ya nyumba kwenye baadhi ya magereza na kujenga nyumba mpya. Mahitaji ya nyumba hivi sasa ni nyumba 14,500 wakati zilizopo ni 4,221 hivyo kuwepo kwa upungufu wa takribani nyumba 10,279 ambao unalazimisha baadhi ya Askari wa Magereza kuishi nje ya kambi za jeshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Magereza limesaini mkataba na kampuni ya Poly Technologies ya China kwa kujenga nyumba 9,500 kwenye vituo vyote vya magereza nchini. Mgawanyo wa ujenzi wa nyumba hizo ni Makao Makuu Magereza nyumba 472, Mkoa wa Arusha nyumba 377, Dar es salaam 952, Dodoma 356, Kagera 364, Kigoma 272, Kilimanjaro 390, Lindi 233, Manyara 206, Mara 378, Mbeya 622, Iringa 336, Morogoro 669, Mtwara 215, Mwanza 398, Pwani 384, Rukwa 358, Ruvuma 320, Shinyanga 337, Singida 299, Tabora 408, Tanga 382, KMKGM Dar es Salaam 219, Chuo cha Ukonga 115, Chuo cha Kiwira 183, Chuo cha Ruanda 62, Chuo cha KPF 27, Bohari Kuu 82 na Bwawani 84.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Jeshi la Polisi, Serikali inakusudia kujenga nyumba 4,136 katika Mikoa 17; hii Mikoa 17 tunayozungumzia, tafsiri yake ni kwamba Mikoa 15 ya Tanzania Bara na Mikoa mitano ya Zanzibar, wameichukulia Unguja na Pemba kama Mkoa kitu ambacho siyo sahihi. Kwa hiyo usahihi wake ni kwamba Mikoa 15 ya Tanzania Bara na Mikoa 5 ya Zanzibar inafanya kuwa Mikoa 19 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nimeona nifanye marekebisho kwa sababu mara nyingi tumekuwa tukizungumza hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali itaendelea kutatua changamoto za uhaba wa nyumba kwa kutumia njia mbalimbali ikiwemo mikopo yenye riba nafuu, miradi shirikishi na kwa kutumia fedha za bajeti ya Serikali kadri hali ya uchumi itakapokuwa ikiimarika. Mkakati huu unakwenda sambamba na mipango ya maendeleo ya Serikali ikilenga kufikia idadi ya nyumba za makazi kwa askari wote waliopo sasa na watakaoajiriwa baadaye.