Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 10 Sitting 4 Youth, Disabled, Labor and Employment Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu 48 2023-02-03

Name

Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Primary Question

MHE. LUHAGA J. MPINA aliuliza: -

Je, ni Vijana wangapi hawana ajira nchini na Serikali imewaandaaje kushindana katika soko la ajira ndani na nje ya nchi?

Name

Paschal Katambi Patrobas

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, (KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Luhaga Joelson Mpina, Mbunge wa Kisesa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, utafiti wa watu wenye uwezo wa kufanya kazi wa mwaka 2021 unaonesha kuwa vijana wenye umri wa miaka 15-35 ambao wana ukosefu wa ajira ni 1,732,509. Idadi hiyo ni sawa na asilimia 12.2 ya nguvu kazi, maana ya vijana walio katika umri huo na wapo katika mfunzo au hawana ulemavu unaosababisha wasijishughulishe na shughuli za kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Katika kuhakikisha kwamba Vijana wanaendelezwa ipasavyo kushindana katika soko la ajira la ndani na nje ya nchi, Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeweka mkakati wa kitaifa wa kukuza ujuzi wa miaka 10 mwaka 2016/2017 – mwaka 2025/2026. Kupitia mkakati huu, Serikali imefanya maboresho ya miundombinu ya mitaala katika ngazi za Elimu ya Juu, Elimu ya Kati, na Mafunzo Stadi ya Ufundi.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, sambamba na maboresho hayo, Serikali imetoa mafunzo ya kuwezesha vijana walio nje ya mafunzo rasmi ili kumudu ushindani katika soko la ajira, yakiwemo mafunzo ya uanagenzi, mafunzo ya uzoefu wa kazi (internship) kwa wahitimu, mafunzo ya urasimishaji ujuzi uliopatikana nje ya mfumo rasmi wa elimu (RPL), na mafunzo ya kilimo cha kisasa kwa kutumia teknolojia ya vitalu nyumba. Ahsante.