Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 5 Enviroment Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira na Muungano 42 2022-04-12

Name

Omar Ali Omar

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Wete

Primary Question

MHE. OMAR ALI OMAR aliuliza: -

Je, Serikali imejipanga vipi kukabiliana na uharibifu unaotokana na ukataji mikoko na uvunaji wa matumbawe ili kuvinusuru visiwa visitoweke?

Name

Khamis Hamza Khamis

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Uzini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Omar Ali Omar, Mbunge wa Wete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na changamoto iliyoainishwa na Mheshimiwa Mbunge Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar zimekuwa zikichukua juhudi mbalimbali za kisera, kisheria pamoja na kuandaa miongozo mbalimbali ya utunzaji wa mazingira ya baharini ili kuhakikisha uharibifu wa mazingira ya bahari unadhibitiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa juhudi hizo ni kama zifuatazo: -

Kwanza, kujenga uelewa kwa wanajamii juu ya utunzaji wa mazingira na rasilimali za bahari ikiwemo uhifadhi wa mikoko na matumbawe.

Pili, upandaji wa mikoko na matumbawe katika maeneo yaliyoathirika kwa kutumia njia mbalimbali endelevu na za kitaalamu. Kwa mfano upandaji wa hekta Saba za mikoko Unguja na hekta 10 Pemba kwa mwaka 2020 – 2021 pamoja na kuweka matumbawe bandia 90 Unguja na Pemba.

Jambo lingine ni ushirikishwaji wa jamii katika kusimamia maeneo ya mikoko na matumbawe ikiwemo kuanzisha hifadhi ndogondogo za kijamii katika maeneo ya Kukuu, Fundo, Makoongwe kwa Kisiwa cha Pemba na maeneo ya Mtende, Tumbatu na Kizimkazi kwa upande wa Kisiwa cha Unguja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru.