Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 14 Education, Science,Technology and Vocational Training, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia 165 2022-02-18

Name

Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Primary Question

MHE. EDWIN E. SWALLE aliuliza: -

Je, tangu kuanzishwa kwa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu, kuna changamoto gani katika kukuza na kuendeleza Mfuko wa Elimu ya Bodi ya Mikopo ili kukopesha wanafunzi wengi zaidi?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Edwin Enosy Swalle, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni azma ya Serikali kukuza na kuendeleza Mfuko wa Elimu ya Bodi ya Mikopo ili kukopesha wanafunzi wengi zaidi. Katika kutimiza azma hiyo, Serikali imekuwa ikiongeza fedha za bajeti ya mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu kila mwaka. Kwa mfano, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali ilitoa kiasi cha shilingi bilioni 570 kwa ajili ya mikopo ya wanafunzi wa Elimu ya Juu ikiwa ni ongezeko la shilingi bilioni 106 kutoka shilingi bilioni 464 ya mwaka 2020/2021.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hizo za Serikali, kumekuwepo na changamoto kadhaa katika kukuza na kuendeleza Mfuko wa Elimu ya Bodi ya Mikopo ambazo zinazotokana na mambo yafuatayo; jambo la kwanza baadhi ya wanufaika wa mikopo iliyoiva kutojitokeza na kurejesha kwa hiari mara baada ya kumaliza masomo. Lakini kambo la pili baadhi ya waajiri kutowasilisha kwa wakati orodha ya waajiriwa wapya ambao ni wanufaika wa mikopo na wengine kuchelewa kuwasilisha makato ya fedha kwa wakati kutokana na wanufaika ambao ni waajiriwa wao.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Bodi ya Mikopo imeendelea kutoa elimu kwa wanufaika na waajiri ili kuhamasisha urejeshaji wa mikopo kwa hiari na kwa kuzingatia matakwa ya kisheria. Vilevile imeendelea kuimarisha kaguzi kwa waajiri pamoja na kuwashirikisha wadau wa kimkakati kama BRELA na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ili kubaini wanufaika wapya na kuongeza kasi ya urejeshaji mikopo iliyoiva kwa lengo la kukuza na kuendeleza Mfuko wa Elimu ya Bodi ya Mikopo ili kukopesha wanafunzi wengi zaidi. Nakushukuru. (Makofi)