Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 14 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 164 2022-02-18

Name

Abeid Ighondo Ramadhani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Primary Question

MHE. ABEID R. IGHONDO aliuliza: -

Wananchi wa Kata za Mgori, Mughungu na Ngimu Jimbo la Singida Kaskazini wapo tayari kukabidhi Msitu wa Mgori kwa Serikali kuwa Hifadhi ya Taifa: -

Je, mchakato wa Serikali kukamilisha zoezi hilo umefikia wapi na faida gani wananchi watazipata kwa msitu huu kuwa hifadhi?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abeid Ramadhani Ighondo, Mbunge wa Singida Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Maliasili na Utalii inapenda kupongeza jitihada zote zilizochukuliwa na Serikali katika ngazi ya Vijiji, Wilaya na Mkoa pamoja na Mheshimiwa Mbunge katika kuhakikisha Msitu wa Mgori ambao ni makazi ya wanyamapori wadogo na wakubwa hususani tembo unahifadhiwa.

Mheshimiwa Spika, hatua iliyofikia mpaka sasa ni mchakato wa kupata Tangazo la Serikali ili kuutambua msitu huo kama hifadhi. Rasimu ya kwanza ya Tangazo la Serikali imetolewa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali tarehe 4 Februari, 2022. Tangazo hilo litadumu kwa siku 90 kabla ya kutolewa tangazo la mwisho ambalo litatoa idhini kwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kusimamia msitu huo.

Mheshimiwa Spika, faida za kuhifadhi msitu huu wenye ukubwa wa hekta 49,000 ni pamoja na: -

(i) Kuweka hali ya hewa nzuri kwa Mkoa wa Singida wenye misitu michache sana ya hifadhi na kuwezesha upatikanaji wa mvua hivyo kusaidia kwenye ukuaji wa sekta nyingine kama kilimo, ufugaji na maji;

(ii) Lakini vilevile utunzaji wa mazingira na vyanzo vya maji;


(iii) Lakini pia uwepo wa baioanuai nyingi za mimea ya asili na makazi ya wanyamapori kama tembo na wengine hivyo, kuchochea shughuli za utalii;

(iv) Sambamba na hilo kuwepo kwa fursa za ufugaji nyuki kwa wenyeji ili kuwaongezea kipato.