Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 10 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 117 2022-02-14

Name

Jacqueline Kandidus Ngonyani (Msongozi)

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha bei ya mbolea inashuka hadi kufikia kiwango cha Wakulima kumudu kuinunua ili kuiepusha nchi yetu kukumbwa na janga la njaa?

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Answer

WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, lenye eneo (a), (b) na (c), kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inakiri kwamba bei ya mbolea katika Soko la Dunia na hapa nchini imepanda kwa msimu wa mwaka 2021/2022 ikilinganishwa na msimu wa mwaka 2020/2021. Kupanda huko kwa bei hakutokani na Serikali au wafanyabiashara wa ndani kupandisha bei, bali kumetokana na kupanda kwenye Soko la Dunia na wakulima wote duniani wameathirika na upandaji huo uliotokana na athari za UVIKO. Mfano, hadi kufikia mwezi Januari, 2022 bei ya Urea ni Dola za Kimarekani 700 kwa tani ikilinganishwa na Dola za 350 kwa msimu wa 21, sawa na ongezeko la asilimia 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto za kupanda kwa bei za mbolea nchini, Serikali inachukua hatua za muda mfupi na muda mrefu. Hatua za muda mfupi zilizochukuliwa mpaka sasa ni pamoja na kununua mazao ya nafaka kwa bei ya juu kuliko bei ya soko ambapo mahindi yalinunuliwa kwa bei ya shilingi 500 badala ya 200.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kuhakikisha kwamba bandari zetu zinatoa kipaumbele cha kushusha mbolea ili kupunguza tozo za bandarini, ununuzi wa mbolea kwa mfumo wa (BPS) katika baadhi ya mazao mfano Tumbaku. Matumizi ya reli kusafirisha mbolea katika maeneo ambapo reli inapita. Matumizi ya mbolea mbadala kama NPS na NPS-Zinc na kuruhusu ushindani kwenye uagizaji wa mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua za muda mrefu zilizochukuliwa ni pamoja na kuhamasisha uwekezaji katika viwanda vya mbolea. Kutokana na uhamasishaji huo, Kampuni ya Itracom Fertilizers kutoka Burundi inaendelea na ujenzi wa kiwanda cha mbolea Mkoani Dodoma chenye uwezo wa kuzalisha tani 600,000 za mbolea na tani 300,000 za chokaa kwa mwaka. Wawekezaji wengi zaidi wanaendelea kujitokeza kutoka nchi mbalimbali kama vile Misri na Saudi Arabia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekutana na uongozi wa kiwanda cha mbolea cha Minjingu kujadili namna kiwanda hicho kinavyotakiwa kuzalisha mbolea kulingana na mahitaji ya udongo na kuongeza uzalishaji wa mbolea kutoka tani 30,000 hadi kufika 100,000 kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara inatambua umuhimu wa mbolea katika uzalishaji wa mazao ya chakula ili kuihakikishia nchi Usalama wa Chakula. Kutokana na tathmini iliyofanyika ambayo iliangalia changamoto hii pamoja na utabiri wa mvua, ulioonesha hatutapa mvua nyingi kwa miaka miwili iliyopita, bado maoteo ya uzalishaji yanaonesha nchi itaweza kujitosheleza katika chakula. Mpaka sasa maeneo mengi ya nchi yanaendelea kupata mvua nzuri. Matumizi ya mbolea yapo kwenye asilimia 50 ya kawaida ya mazao ya shambani. Kwa hali hiyo, Wizara ya Kilimo inapenda kuwahakikishia wananchi kwamba, nchi haitakumbwa na janga la njaa.