Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 9 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 105 2022-02-11

Name

Josephine Johnson Genzabuke

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza: -

Je, Serikali imewezesha kwa kiasi gani Maafisa Ushirika kuweza kufanya shughuli zao kwa ufanisi, ikizingatiwa kuwa kumekuwa na msukumo mkubwa sana wa kuanzisha Vyama vya Ushirika?

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na jitihada za kuhamasisha uanzishwaji wa Vyama vya Ushirika katika sekta mbalimbali nchini ili kujenga umoja na mshikamano katika ukuzaji uchumi wa Watanzania kupitia Ushirika. Jitihada hizo pia hufanyika sambamba na kuweka mazingira wezeshi kwa maafisa ushirika ambao wanalo jukumu la kuhamasisha uanzishwaji na uendelezwaji wa Vyama vya Ushirika. Lakini pia utoaji mafunzo ya usimamizi na uendeshaji wa ushirika kwa viongozi na wanachama wa Vyama vya Ushirika.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2021/ 2022 Serikali kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania ilitenga jumla ya shilingi bilioni 2.7 kwa ajili ya: -

(i) Kununua magari 13 ambayo taratibu za manunuzi zipo katika hatua za mwisho, pikipiki 137 zimenunuliwa ili kuwezesha ofisi za Warajisi Wasaidizi wa Mikoa 26 ya Tanzania Bara kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi;

(ii) Mafunzo ya usimamizi wa Vyama vya Ushirika nchini kwa Maafisa Ushirika 184 yametolewa;

(iii) Kutoa mafunzo ya uendeshaji wa Vyama vya Ushirika kwa maafisa ushirika 100;

(iv) Kuunda Mfumo wa TEHAMA utakaowezesha ufuatiliaji na usimamizi wa Ushirika nchini; na

(v) Kuendelea na kazi za usimamizi na kaguzi za mara kwa mara katika Vyama vya Ushirika 9,185.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuhakikisha kwamba elimu ya kutosha inatolewa kwa viongozi na wanachama wa Vyama vya Ushirika nchini. Aidha, Serikali haitasita kuwachukulia hatua kali viongozi wote wasio na uadilifu ili kuwezesha wanachama wa Ushirika wananufaika na ushirika wao.