Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 19 Health and Social Welfare Ofisi ya Rais TAMISEMI. 156 2016-05-13

Name

Cosato David Chumi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafinga Mjini

Primary Question

MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:-
Hospitali ya Mji wa Mafinga inahudumia wakazi wa Halmashauri ya Mji wa Mafinga na Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi na pia Wilaya jirani za Mbarali na Iringa Vijjini lakini pia iko kandokando ya barabara kuu, hivyo kukabiliwa na mzigo mzito wa kuhudumia majeruhi wa ajali zinazotokea kwenye barabara hiyo kama ile ya Mafinga:-
Je, Serikali iko tayari kuiongezea hospitali hiyo fedha na watumishi mara mbili zaidi ya kiwango inachopata sasa iweze kuwa na uwezo wa kutosha kukabiliana na mzigo wa kazi?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikiipatia hospitali hii fedha kwa ajili ya kuendesha huduma ambako kwa mwaka wa fedha 2016/2017, fedha zilizotengwa ni shilingi milioni 90 kwa ajili ya maendeleo na shilingi milioni 90 kwa ajili ya matumizi mengineyo. Aidha, katika kuongeza wigo wa upatikanaji wa fedha za uboreshaji huduma za afya, Serikali imesisitiza umuhimu wa kila Halmashauri kuboresha makusanyo ya ndani kupitia mifumo ya afya ya jamii yaani CHF/TIKA na fedha za makusanyo mengine kwa kutumia mifumo ya kielektroniki ili kuongeza uwezo wa kutoa huduma katika hospitali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu watumishi, Hospitali ya Wilaya ya Mafinga ina jumla ya watumishi 209, upungufu ikiwa ni watumishi 95 sawa na asilimia 31.3. Kwa mwaka wa fedha 2016/2017, Halmashauri imeidhinishiwa kuajiri watumishi 18 na itaendelea kuongeza idadi hiyo kila mwaka ili kukidhi mahitaji ya hospitali hiyo.