Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 6 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 65 2022-02-08

Name

Salim Mussa Omar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Gando

Primary Question

MHE. SALIM MUSSA OMAR aliuliza:-

Je, ni nini kinachosababisha mabadiliko makubwa ya bei za tiketi za ndege za Air Tanzania kwa safari za Dar es Salaam na Dodoma ambapo mara nyingi hufika hadi shilingi laki sita?

Name

Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ileje

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Salim Mussa Omar, Mbunge wa Gando, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo wa uuzaji wa tiketi katika biashara ya usafiri wa anga ni mojawapo ya mikakati ya ushindani ili kuvutia wateja. Mashirika ya Ndege hushindana kwa kutumia mkakati huu ambapo tiketi hupangwa katika ngazi mbalimbali kufuatana na vigezo mbalimbali kama vile bei ya tiketi, ujazo wa ndege, muda wa kukata tiketi, masharti ya tiketi na daraja la usafiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutumia kigezo cha ujazo wa ndege na muda ambao abiria anakata tiketi, mteja anayekata tiketi mapema na kukuta ndege haijajaa hupata bei ya chini ukilinganisha na mteja anayekata tiketi muda mfupi kabla ya safari yake na kukuta ndege imejaa, ambapo mara nyingi huwa siku chache au muda mfupi kabla ya safari, hupata bei za juu. Mfumo huu unatumika Kimataifa na mashirika yote ya ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ATCL bei hizi zimepangwa katika ngazi mbalimbali. Kwa mfano, katika safari ya Dodoma kwenda na kurudi, ATCL ina jumla ya ngazi 13 katika daraja la kawaida (economy class) ambapo bei zake zinaanzia shilingi 331,400/= hadi shilingi 678,400/=. Bei ya juu ya wastani wa shilingi 600,000/= ni viti 10 kati ya jumla ya viti 76 vya ndege nzima sawa na takribani asilimia 13 ya ujazo wa ndege. Hivyo, abiria wakiwahi kukata tiketi wana nafasi kubwa ya kupata bei za chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, kuna daraja la biashara (business class) ambalo kuna viti sita tu na ni kwa abiria yeyote ambaye yupo tayari kulipa katika daraja hilo. Daraja hilo linatoa huduma maalum, kwa mfano, mteja anapewa kilo saba zaidi za mzigo ukilinganisha na daraja la kawaida, mteja hupatiwa mhudumu wa kumsikiliza kwa haraka muda wowote akiwa ndani ya ndege, mteja kutokuwa na gharama za kubadilisha safari akifanya mabadiliko hayo kwa mara ya kwanza na pia mteja hupewa kipaumbele wakati wote wa safari kuanzia wakati wa ukaguzi (check in). Kutokana na sababu hizi, gharama za daraja hili ni kubwa kuliko daraja la kawaida. Daraja hili la biashara lina ngazi nne zenye bei kati ya shilingi 721,600/= hadi shilingi 953,000/=.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na maelezo hayo, namwelekeza Mkurugenzi Mtendaji wa ATCL kufanya utafiti wa nauli zinazotozwa na mashirika ya ndege washindani kwa safari za ndani ili kuziwianisha na kisha kupanga nauli zinazoweza kuvutia Watanzania wengi kutumia ndege za ATCL. Ahsante. (Makofi)