Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 5 Energy and Minerals Wizara ya Madini 49 2022-02-07

Name

Sophia Hebron Mwakagenda

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA Aliuliza: -

Je, ni lini mgodi wa makaa ya mawe Kiwira utapata Mwekezaji mpya na kulipa mafao ya waliokuwa wafanyakazi wa mgodi huo?

Name

Doto Mashaka Biteko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukombe

Answer

WAZIRI WA MADINI Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda, Mbunge Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Shirika limeamua kuchukua hatua za ndani za kuendesha mgodi wa Kiwira kwa kuchukua hatua mahsusi za kuendeleza mradi wa Kiwira kwa ajili ya uwekezaji mkubwa wa kuzalisha umeme wa MW 200 badala ya kutafuta mwekezaji mpya. Hatua hizo ni pamoja na kufanya ukarabati wa miundombinu ya mgodi, kuboresha barabara, kurejesha njia za reli katika mgodi wa chini (underground mine), mifumo ya hewa, maji na matengenezo ya mikanda ya kusafirishia makaa kuja nje ya mgodi.

Mheshimiwa Spika, hatua hii ni kuwezesha kuchimba makaa ya mawe kwa wingi kwa ajili ya kuzalisha umeme na matumizi mengine. Ukarabati wa miundombinu ya mgodi huu umefikia asilimia 98. Aidha, hatua nyingine iliyochukuliwa na Serikali ni kuanzisha ushirikiano kati ya STAMICO na TANESCO. Katika ushirikiano huo, STAMICO itahusika na uzalishaji wa makaa ya mawe kwa ajili ya matumizi kwenye kinu cha umeme (power plant) na TANESCO itahusika na ujenzi wa kinu cha kuzalisha umeme pamoja na miundombinu yake. Kadhalika, TANESCO watahusika na uzalishaji na usambazaji wa umeme kwa wananchi kwa kujenga njia ya umeme yenye urefu wa km 100 kutoka kwenye mgodi huo.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa mgodi unaendelea na uchimbaji wa makaa ya mawe kwa matumizi ya viwanda katika eneo la Kabulo. Makaa hayo yanauzwa kwenye viwanda mbalimbali vya saruji nchini.

Mheshimiwa Spika, kuhusu malipo ya mafao ya waliokuwa wafanyakazi wa mgodi wa Kiwira, Wizara ya Fedha na Mipango inayafanyia kazi kufuatia kukamilika kwa uhakiki wa madai hayo ambayo yanahusisha stahiki na mapunjo ya watumishi waliokuwa wafanyakazi wa Mgodi wa Kiwira baada ya Mgodi huo kusimamisha uzalishaji wake mwaka 2007. Aidha, katika kipindi hicho mgodi ulikuwa unaendeshwa na kampuni binafsi ya TANPOWER na mwaka 2013 mgodi huo ulikabidhiwa Serikalini kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO).