Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 5 Investment and Empowerment Wizara ya Viwanda , Biashara na Uwekezaji 44 2022-02-07

Name

Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NG’WASI D. KAMANI Aliuliza: -

Je, Serikali imefikia hatua gani katika kuunganisha Mifuko ya Uwezeshaji Wananchi hususan Vijana na kuwa na eneo moja la wazi la utoaji huduma?

Name

Exaud Silaoneka Kigahe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwa ridhaa yako kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu anayetujalia uhai tuendelee kutekeleza majukumu yetu ya kila siku. Lakini pili, nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu mpenda wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuniamini na kuweza kuniendeleza kubaki katika nafasi ya Naibu Waziri katika Wizara hii ya Uwekezaji Viwanda na Biashara, ili niweze kuendelea kumsaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ng’wasi Damas Kamani, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara inasimamia Sera ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya Mwaka 2004 na Sheria ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya mwaka 2004. Aidha, Serikali inaratibu utekelezaji wa mifuko na programu za uwezeshaji 62 ambapo mifuko na proramu 52 zinamilikiwa na Serikali na mifuko na programu 10 zinamilikiwa na taasisi za sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, kati ya mifuko hiyo na proramu 52 zinazomilikiwa na Serikali, mifuko 21 inatoa mikopo ya moja kwa moja kwa walengwa, mifuko tisa inatoa dhamana ya mikopo, mifuko 17 inatoa ruzuku na programu tano ni za uwezeshaji ambazo zinatoa huduma mbalimbali ikiwemo ujenzi, urasimishaji ardhi na uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa hii kulijulisha Bunge lako tukufu kuwa, Serikali ipo katika hatua za mwisho za kukamilisha taarifa ya tathmini ya mifuko hiyo na taarifa hiyo itawasilishwa hapa Bungeni baada ya kukamilika. Nakushukuru sana.