Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 4 Youth, Disabled, Labor and Employment Ofisi ya Waziri Mkuu: Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu 26 2022-02-04

Name

Ali Hassan Omar King

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Jang'ombe

Primary Question

MHE. ZAYTUN S. SWAI K.n.y. MHE. ALI HASSAN OMAR KING aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawatambua watoto wenye ulemavu ambao wanaishi kwenye mazingira magumu ili kuwasaidia kwa matibabu na kimaisha?

Name

Paschal Katambi Patrobas

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ali Hassan King, Mbunge wa Jang’ombe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuwatambua na kuwapatia huduma stahiki watu wenye ulemavu ikiwa ni pamoja na waishio katika mazingira hatarishi zaidi kwa kuzingatia aina ya ulemavu walionao na hitaji la msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utambuzi huo umekuwa ukifanyika kwa kuzingatia Sera ya Taifa ya Maendeleo na Huduma kwa Watu wenye Ulemavu ya mwaka 2004. Kwa kuzingatia sera hiyo, Serikali imeanzisha Rejesta ya Utambuzi wa Watoto Waishio katika Mazingira Hatarishi zaidi. Serikali imeweka pia mfumo wa ulinzi na usalama wa watoto. Aidha, Serikali imekamilisha Mwongozo wa Utambuzi wa Mapema wa Afua na Stahiki za Watoto wenye Ulemavu wa mwaka 2021 unaoainisha namna sahihi ya kumtambua mtoto mwenye ulemavu na afua anazostahili kupatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto wenye ulemavu waishio katika mazingira hatarishi zaidi hupatiwa huduma kupitia afua mbalimbali ikiwemo kupatiwa elimu kupitia shule zenye vitengo maalum na jumuishi; kuwapeleka katika hospitali kwa ajili ya kupatiwa afua za matibabu, kupatiwa stadi za maisha kwa lengo la kuwajengea uwezo ili waweze kujitegemea na kujilinda; kupatiwa uchangamshi wa awali na huduma za utengamao; kuwarejesha katika familia zao na kuwaweka katika familia za kuaminika (fit family); utoaji wa vifaa saidizi; kuwaunganisha na vyuo maalum vya watu wenye ulemavu kwa ajili ya kupatiwa ujuzi na huduma za marekebisho na kwa wale ambao hawana walezi au wazazi hupelekwa kwenye makao ya watoto kwa ajili ya huduma mbalimbali.