Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 3 Health and Social Welfare Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum 19 2022-02-03

Name

Neema Kichiki Lugangira

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA Aliuliza: -

Je, Serikali haioni haja ya kuja na mpango mkakati wa kuwezesha NGOs kupata rasilimali fedha kupitia njia mbalimbali ikiwemo ruzuku katika maeneo mahsusi kama ambavyo inafanyika kwa Vyama vya Siasa, hasa baada ya uamuzi wa Serikali kuanzisha Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum ambayo inahusisha Asasi za Kiraia katika malengo yake?

Name

Dr. Dorothy Onesphoro Gwajima

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM Alijibu: -

Mheshimwa Mwenyekiti, ahsante sana. awali ya yote kwa ridhaa yako naomba niseme maneno machache tu kwa sababu hii ni Wizara mpya.

Mheshimwa Mwenyekiti, kwanza, naomba kutoa shukrani zangu za pekee kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa maono yake makubwa ya kuunda Wizara hii mpya itakayoshughulikia masuala ya maendeleo ya jamii, jinsia, wanawake na makundi maalum.

Mheshimwa Mwenyekiti, hakika maono yake yamekuja kwa wakati ambapo kwa sasa kasi ya maendeleo kupitia msukumo wa teknolojia ni kubwa na changamoto za nchi yetu ni nyingi katika makundi mbalimbali ya jamii zetu, jambo ambalo linahitaji chombo mahususi cha kuangalia kwa kina zaidi changamoto hizi na fursa zilizopo ili kuweza kuiendeleza jamii yetu.

Mheshimwa Mwenyekiti, aidha, namshukuru kwa imani yake kwangu kuendelea kuniamini na kuniteua niweze kuisimamia Wizara hii. Mimi na timu yangu yote ambayo ametuamini tunaahidi hatutamuangusha. Tutaungana na jamii na wadau wote kuhakikisha tunaleta msukumo wenye tija kuendeleza maono aliyonayo na jamii yetu kuweza kuendelea na kuwa na ustawi.

Mheshimwa Mwenyekiti, baada ya hayo, naomba nijielekeze kwenye swali la Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, Mbunge wa Viti Maalum. Majibu ya swali hili ni kwamba: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa sasa haijatenga fungu maalum kwa ajili ya ruzuku kwa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali. Hata hivyo, Serikali kwa kutambua umuhimu wa mashirika hayo kuwa uendelevu, tarehe 30 Septemba, 2021 Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, aliagiza Wizara kwa kushirikiana na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali na wadau mbalimbali kuandaa Mpango Mkakati wa kuwezesha mashirika haya kupunguza utegemezi. Rasimu ya andiko la awali la Mpango huu imeandaliwa ambayo imeainisha njia mbalimbali za kuwezesha Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kuweza kupata rasilimali za kutekeleza shughuli zao. Ahsante.