Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 2 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 13 2022-02-02

Name

Sylivia Francis Sigula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SYLVIA F. SIGULA aliuliza: -

Je, nini mpango wa Serikali wa kutoa ajira rasmi na zisizo rasmi kupitia tasnia ya Sanaa?

Name

Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Answer

WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hii ni mara yangu ya kwanza kusimama kwenye Bunge lako hili Tukufu katika Wizara hii mpya ya Utamaduni Sanaa na Michezo, nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema na mjawa wa kadiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, namshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniamini kwa mara nyingine na kuniteua katika Wizara hii. Naomba nimthibitishie Mheshimiwa Rais kwamba Wizara yetu hii pamoja na watendaji wa Wizara tutajipanga kweli kweli ili matamanio yake aliyokusudia katika Wizara hii yaweze kutimia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Sylvia Francis Sigula, kwanza kwa kutambua mchango wake kwa vijana. Amekuwa na mchango mzuri kwa vijana, nasi kama Wizara tunampongeza sana kwa kuwasemea vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kwa kutambua kwamba swali lake ni la msingi na la muhimu sana, ili kuwavutia wadau hasa vijana kujiajiri katika Sekta ya Sanaa, mpango wa Serikali ni kuendelea kuboresha mazingira ya kazi za sanaa kwa kufanya mambo kadhaa. Moja ya mambo makubwa ambayo tunakwenda kuyafanya ni: -

Kwanza, ni kuhakikisha vifaa na vitendea kazi vya sanaa vinapatikana kwa bei nafuu kwa kufanya mapitio kwenye kodi za vifaa husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, tutakwend kupitia upya tozo kwenye Kanuni za BASATA, COSOTA na Bodi ya Filamu Tanzania ili ziwe rafiki kwa walipaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, tutakwenda kuanzisha mifumo mbalimbali ya kieleketroniki ya usajili, ambayo mingine tunayo lakini tutakwenda kubuni na kuendeleza mingine ya maombi ya vibali na leseni pamoja na mfumo rasmi wa ukusanyaji mirabaha kutoka kwa watumiaji wa kazi za sanaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, tutakwenda kujenga miundombinu ya sanaa kama vile Arts Arena, National Art Gallery na One Stop Center, ambayo tayari tunayo inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, tunakwenda kuanzisha Mfuko ambao utakaokuwa ni suluhisho la kimitaji na mafunzo kwa wadau wa Sekta ya Sanaa.