Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 9 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 98 2021-11-12

Name

Charles John Mwijage

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba Kaskazini

Primary Question

MHE. CHARLES J. P. MWIJAGE aliuliza: -

Nchi yetu imekuwa na mipango mkakati wa kuzalisha mafuta ya kula kiasi cha kutosheleza soko la ndani.

(a) Je, ni kwa nini Serikali isiboreshe mpango ya kuzalisha mafuta ya mawese kimkakati kwa kuhamasisha kilimo cha zao hilo katika Mikoa ya Kagera, Tanga, Pwani, Katavi na Mbeya?

(b) Je, ni kwa nini Serikali isitumie mfumo wa kilimo kikubwa cha pamoja (block farming) ambapo Serikali hubeba gharama za awali na hatimaye sehemu ya gharama hukatwa kwenye mauzo ya Mkulima?

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Kilimo naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Charles John Mwaijage, Mbunge wa Muleba Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Kilimo kwa kushirikiana na Sekretarieti za Mikoa ya Kagera, Tanga, Pwani, Katavi na Mbeya na Halmashauri za Mikoa hiyo inaendelea kuhamasisha uzalishaji wa zao la michikichi katika maeneo yanayofaa kuzalisha zao hilo.

Uhamasishaji huo ni pamoja na kuzitaka Halmashauri hizo kuanzisha vitalu vya kuzalisha miche bora ya michikichi aina ya Tenera, kutoa mafunzo kwa wakulima na wataalam kuhusu kilimo bora cha michikichi na kuhamasisha uanzishwaji wa viwanda vidogo na vya kati vya kuchakata mafuta ya mawese jirani na maeneo ya uzalishaji ili kusafirisha mikungu ya michikichi kwenda viwandani.

Mheshimiwa Spika, kutokana na uhamasishaji huo baadhi ya Halmashauri za Wilaya zimeanzisha vitalu vya kuzalisha miche bora ambapo Ngara (Kagera) imeanzisha kitalu cha miche 100,000; Mkuranga (Pwani) miche 20,000; Tanganyika (Katavi) miche 70,000 na Kyela (Mbeya) miche 26,600.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Halmashauri zenye maeneo makubwa yanayofaa kwa kilimo cha michikichi inaendelea kuhamasisha kilimo cha mashamba ya pamoja (Block farming) ili kuzalisha kwa tija na kurahisisha huduma kwa wakulima. Baadhi ya Halmashauri hizo ni Uvinza (Kigoma) ekari 5,000 na Uyui (Tabora) ekari 12,000. Uhamasishaji unaendelea kwa mikoa mingine yenye sifa hizo.