Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 5 Foreign Affairs and International Cooperation Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 58 2021-11-08

Name

Ritta Enespher Kabati

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. RITHA E. KABATI aliuliza: -

(a) Je Serikali inayo database ya kutambua idadi ya Watanzania wanaoishi nje ya nchi?

(b) Je nini mchango wa Watanzania wanaoishi nje ya Tanzania katika kipindi cha miaka mitano?

Name

Amber. Mbarouk Nassor Mbarouk

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitumia mifumo mbalimbali ya kutambua Watanzania wanaoishi nje ya nchi, ikiwa ni pamoja na usajili wao kupitia Balozi zetu na Idara ya Uhamiaji kwa kutumia usajili wa hati za kusafiria za kielektroniki. Hadi kufikia Januari, 2021 idadi ya Watanzania wapatao Milioni moja na Laki Mbili (1,200,000) wanaishi nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, Watanzania wanaoishi nje ya Tanzania wamekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa letu. Kwa mfano katika kipindi cha miaka mitano iliyopita michango yao imehusisha sekta mbali mbali zikiwemo; Sekta ya Fedha, Sekta ya Afya na Sekta ya Nyumba. Mfano, takwimu za Benki Kuu ya Tanzania (BoT) zinaonesha fedha za kigeni (remittance) ambazo zimetumwa kupitia mfumo rasmi kutoka kwa Watanzania wanaoishi nje ya Tanzania kwa kipindi cha miaka mitano ni takriban Dola za Kimarekani bilioni 2.3 sawa na shilingi za Tanzania trilioni 5.3.

Mheshimiwa Spika, aidha, michango ya Watanzania wanaoishi nje ya nchi katika Sekta ya Afya kwa kipindi cha miaka mitano inahusisha utoaji wa vifaa tiba, madawa, vitabu vya masuala mbalimbali ya afya na mafunzo ya elimu ya afya bora kwa wauguzi na madaktari kwenye hospitali za Tanzania Bara na Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa Sekta ya Nyumba Watanzania wanaoishi nje ya Tanzania kwa kipindi cha miaka mitano wamenunua nyumba zaidi ya 135 zenye thamani ya shilingi za Tanzania bilioni 29.7 kupitia Shirika la Nyumba la Taifa (NHC). Ahsante sana.