Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 2 Water and Irrigation Wizara ya Maji 21 2021-11-03

Name

Aida Joseph Khenani

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itamaliza changamoto ya maji katika Jimbo la Nkasi Kaskazini?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Joseph Khenani, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, upatikanaji wa huduma ya majisafi na salama katika Wilaya ya Nkasi ni wastani wa asilimia 52.2. Katika kutatua changamoto ya huduma ya majisafi na salama katika Jimbo la Nkasi Kaskazini, Serikali imeendelea na utekelezaji wa miradi minne ambayo ni Kirando, Namanyere, Matala na Katongolo. Miradi hii imepangiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Desemba, 2021.

Mheshimiwa Spika, aidha, kuanzia mwezi Januari, 2022 Serikali itaanza utekelezaji wa miradi ya maji katika Vijiji vya Korongwe, Lyazumbi, Masolo, Mpata, Isale na Kakoma na utekelezaji wa miradi hiyo umepangwa kukamilika mwezi Oktoba, 2022. Kukamilika kwa miradi hiyo, kutawanufaisha wananchi wapatao takribani 97,000.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Mji wa Namanyere, Serikali inaendelea na uboreshaji wa huduma ya majisafi na salama kwa kutumia chanzo cha maji cha Bwawa la Mfili. Ujenzi wa mradi huo unahusisha kazi za ujenzi wa chanzo, ufungaji wa pampu mbili zenye uwezo wa kusukuma lita 80,000 za maji kwa saa, ulazaji wa bomba kuu kilometa 3.9, ulazaji wa bomba la kusambaza maji kilometa 6.4, ujenzi wa tanki la lita 500,000. Ujenzi wa mradi huo umepangwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Desemba, 2021.

Mheshimiwa Spika, aidha, kupitia mradi wa Maziwa Makuu wa kutumia Ziwa Tanganyika, Serikali imekamilisha usanifu wa kina na uandaaji wa makabrasha ya zabuni ya kumpata Mkandarasi wa ujenzi wa mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Tanganyika. Kupitia mradi huo, vijiji 32 vya Halmashauri ya Nkasi vinatarajiwa kunufaika.