Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 1 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 11 2021-11-02

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Primary Question

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itamaliza tatizo sugu la soko la zao la tumbaku nchini?

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, soko la tumbaku linategemea mahitaji katika soko la dunia. Mahitaji ya tumbaku na bidhaa zake yamekuwa yakishuka katika Soko la Dunia kwa wastani wa asilimia sita hadi saba kwa mwaka. Hali hiyo inachangiwa kwa kiasi kikubwa na kampeni ya kidunia ya kupunguza uzalishaji na matumizi ya tumbaku pamoja na bidhaa zake, pamoja kuanza matumizi ya sigara aina mpya inayotumia kilevi cha kutengeneza maabara (Laboratory nicotine) iitwayo e-cigarette.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Bodi ya Tumbaku Tanzania inaendelea kutafuta masoko ya tumbaku kwa kuwashawishi wanunuzi waliopo kuongeza kiwango cha ununuzi kwa njia ya mkataba, kutafuta wanunuzi wapya na pia kutafuta masoko mengine mapya nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, kufuatia hatua hizo, wanunuzi wakubwa wameongeza ununuzi wa tumbaku kutoka kilo 39,000,000 katika msimu wa mwaka 2017/2018 hadi kilo 57,000,000 msimu wa mwaka 2021/2022, sawa na ongezeko la asilimia 46. Serikali imehamasisha wanunuzi wapya na kwa msimu wa 2021 kampuni nane za kizawa zilingia mkataba na wakulima kununua kilo 17,000,000. Katika hatua nyingine Serikali imeendelea kutafuta masoko mapya ambapo, Serikali inaendelea kutafuta soko la China na tayari walileta aina ya tumbaku wanayotaka na majaribio yamefanyika na sampuli ya tumbaku hiyo imepelekwa kwa hatua zaidi.

Mheshimiwa Spika, jitihada za kutafuta masoko zinaendelea katika nchi mbalimbali, Serikali inaamini kuwa baada ya muda mfupi tatizo la soko kwa wakulima wa tumbaku wa Tanzania linaenda kupungua.