Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 8 Works, Transport and Communication Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari 101 2021-09-09

Name

Emmanuel Adamson Mwakasaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Primary Question

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA aliuliza: -

Je, Serikali ina mikakati gani ya ziada ya kudhibiti tatizo la utapeli na wizi wa kimtandao kupitia simu za mkononi?

Name

Kundo Andrea Mathew

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bariadi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Emmanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali tayari imechukua hatua za kuweka mazingira salama kwa wananchi hususan kwenye mitandao kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2015 Serikali ilitunga Sheria ya Makosa ya Mitandao kwa lengo la kutambua kisheria makosa yanayofanyika kwenye mitandao ili kuweza kuchukua hatua stahiki yanapobainika makosa hayo; na vile vile, Sheria ya Miamala ya Kielektroniki kwa lengo la kutambua miamala inayofanyika kimtandao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilianzisha Kitengo cha Uhalifu wa Mitandao chini ya Jeshi la Polisi kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa makosa ya kimitandao ikiwemo wizi wa aina yoyote kwenye mtandao na kuandaa majalada ya kufungulia mashtaka kwa kusaidiana na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka. Watuhumiwa wanaokamatwa kutokana na matumizi mabaya ya mitandao huchukuliwa hatua stahiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, Februari, 2021 Serikali imeunda Kamati ya Taifa ya Kusimamia Utatuzi wa Matumizi Mabaya ya Huduma na Bidhaa za Mawasiliano ambayo inahusisha Wizara na taasisi zote zinazohusika katika kushughulikia makosa ya mtandao. Kamati hiyo ni Kamati ya kudumu na inaishauri Serikali namna ya kutatua changamoto za mitandao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na Watoa Huduma wa Simu za Mkononi imeanzisha mfumo kupitia namba 15040 wa kupokea na kuzifungia namba ambazo zimeripotiwa na kuthibitika kutuma ujumbe au kupiga simu za utapeli. Baada ya kuthibitisha namba hizo kufanya vitendo hivyo, namba husika hufungiwa na kitambulisho cha NIDA kilichotumika kusajili namba hiyo kufungiwa pia, lakini vile vile hata kifaa ambacho kimetumika pia(simu) kinafungiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali itaendelea kuongeza jitihada za kuelimisha Umma matumizi mazuri na sahihi ya TEHAMA kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Ahsante. (Makofi)