Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 62 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 522 2021-06-30

Name

Abdallah Jafari Chaurembo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbagala

Primary Question

MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuyarudisha kwenye Halmashauri maeneo yote yasiyoendelezwa na Mashirika ya Umma kwa zaidi ya miaka kumi ili Halmashauri zijenge miundombinu ya huduma za jamii?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Jafari Chaurembo, Mbunge wa Mbagala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, haki ya kumiliki ardhi hutolewa kwa mujibu wa Sheria za Ardhi. Hivyo zimeweka masharti ya umiliki wa ardhi ikiwa ni kufanya maendelezo ndani ya muda husika, pamoja na hatua za kuchukua endapo kuna ukiukwaji wa masharti hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba baadhi ya Mashirika ya Umma yaliyomilikishwa ardhi katika maeneo mbalimbali nchini, hayajaendeleza ardhi zao. Katika kutatua changamoto hizo, Wizara kwa kushirikiana na mamlaka za upangaji, imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kushughulikia ardhi iliyomilikishwa na kuachwa bila kuendelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Mkoa wa Dar es Salaam, Wizara imeanza kwa kufanya ukaguzi wa maeneo yaliyomilikishwa kwa watu binafsi, wawekezaji wakubwa na Mashirika ya Umma ili kubaini ukiukwaji wa masharti ya umiliki yaliyotolewa na hivyo kuanzisha taratibu za ubatilisho. Baada ya kubatilisha miliki za maeneo ambayo hayajaendelezwa, ardhi husika hupangwa na kupimwa upya kwa ajili ya matumizi mbalimbali ikiwemo uwekezaji, miundombinu ya huduma za jamii kwa kuzingatia mahitaji halisi ya sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa rai kwa Halmashauri zote nchini kuendelea kufanya ukaguzi wa maeneo yaliyotolewa kwa Mashirika, Makampuni na watu binafsi na kuanzisha utaratibu wa ubatilisho endapo itabainika uwepo wa ukiukwaji wa masharti ya umiliki na kuwasilisha mapendekezo Wizarani kwa hatua stahiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.