Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 57 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 483 2021-06-23

Name

Daniel Awack Tlemai

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Karatu

Primary Question

MHE. DANIEL A. TLEMAI aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuendeleza mashamba ya Karatu –Bendhu pamoja na kuwalipa wafanyakazi wa mashamba hayo?

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Awack Tlemai, Mbunge wa Jimbo la Karatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Karatu ina jumla ya mashamba 33 yanayomilikiwa na wawekezaji katika tasnia ya mazao ya biashara na chakula. Kati ya mashamba hayo 33 mojawapo ni Shamba la Bendhu lililopo Kata ya Oldeani lenye ukubwa wa hekta 472, Mwekezaji wa shamba hilo aliyemilikishwa kwa miaka 99 kuanzia 1948 hadi 2047, ameliendeleza kwa asilimia 49 kwa kilimo cha mazao ya ngano na kahawa. Aidha asilimia 45 ya shamba linalimwa na wafanyakazi kwa ajili ya kujikimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya mashamba yote 33, Shamba la Bendhu ndiyo lenye mgogoro wa mirathi iliyotangazwa kupitia Gazeti la Serikali Na.6 la tarehe 5 Februari, 2021 katika ukurasa wa 13. Kutokana na mgogoro huo uzalishaji wa mazao katika shamba hilo uliyumba na kusababisha malipo kwa wafanyakazi kutofanyika kwa wakati. Aidha, wafanyakazi wa shamba hilo walifungua kesi Na.8 ya mwaka 2015 katika Kamisheni ya Usuluhishi na Maamuzi (CMA) Arusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na majadiliano ya kesi hiyo, mwezi Desemba, 2020 yalifikiwa makubaliano kwamba wafanyakazi wataendelea kulipwa kadri ya mapato yatakavyokuwa yanapatikana kutokana na uzalishaji katika shamba hilo. Pia, utekelezaji wa makubaliano hayo unasimamiwa na Chama cha Wafanyakazi. Aidha, nia ya Serikali ni kuona utekelezaji wa makubaliano hayo unafanyika bila changamoto yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na shauri la mirathi kuwa mahakamani, Serikali inasubiri maamuzi ya Mahakama juu ya shauri hilo. Aidha, hakuna migogoro iliyopo katika mashamba mengine 32 ya Karatu. Hata hivyo mkakati wa Serikali ni kuendelea kufuatilia mashamba yote ya uwekezaji yaliyopo Wilayani Karatu na kwingineko nchini ili kuhakikisha mashamba hayo yanaendelezwa na kuzalisha kwa maslahi ya nchi. (Makofi)