Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 57 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 476 2021-06-23

Name

Miraji Jumanne Mtaturu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Mashariki

Primary Question

MHE. MIRAJI J. MTATURU aliuliza: -

(a) Je, ni lini Serikali itajenga Vituo vya Afya vya Issuna, Ikungi, Makiungu, Ntuntu na Misughaa ili kurahisisha huduma za dharura Wilayani Ikungi kwa kuwa Wilaya hii inapitiwa na Barabara ya Dodoma – Mwanza ambayo imekuwa na ajali za mara kwa mara?

(b) Je, ni lini Serikali itapeleka Gari la Wagonjwa ili kuwahisha majeruhi na wagonjwa katika Hospitali za Rufaa?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshmiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi iliyoanza kujengwa mwaka wa fedha 2018/2019 ambapo hadi mwezi Mei 2021 ilikuwa imepatiwa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 800 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa hospitali hiyo. Hospitali hiyo itasaidia kuokoa maisha ya majeruhi wa ajali zitakazotokea eneo la Ikungi katika barabara ya Dodoma hadi Mwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kuanzia mwaka wa fedha 2017/2018 hadi Mei 2021 Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi shilingi milioni 900 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya Ihanja na Sepuka. Ujenzi wa Vituo hivyo umekamilika na vinatoa huduma ikiwemo huduma za dharura za upasuaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inapitia Sera ya Zahanati katika kila Kijiji na Kituo cha Afya katika kila Kata na itafanyiwa maboresho yenye tija zaidi ili ili ujenzi uwe wa kimkakati badala ya kila Kijiji au kila Kata.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya Ikungi ina magari matatu ya kubebea wagonjwa ambayo yapo katika Vituo vya Afya Ikungi, Sepuka na Ihanja ambayo yote yanaendelea kutoa huduma za rufaa za dharura ndani na nje ya wilaya ya Ikungi. Ahsante.