Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 56 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 469 2021-06-22

Name

Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Primary Question

MHE. EDWIN E. SWALLE aliuliza: -

Je, upi mpango wa Serikali katika kukwamua zao la zhai ambalo ni miongoni mwa mazao ya kimkakati yenye changamoto nyingi nchini?

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Edwin Enosy Swalle, Mbunge wa Jimbo la Lupembe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa zao la chai kutokana na mchango wake katika Pato la Taifa, ajira kwa wadau wanaohusika katika mnyororo wa thamani wa zao na kipato kwa wakulima wa chai. Katika kuongeza uzalishaji na tija ya zao la chai, Serikali inaendelea kuwekeza katika utafiti na uzalishaji wa miche bora ya chai ambapo hadi kufikia Mei, 2021, Taasisi ya Utafiti ya TRIT imefanikiwa kuzalisha aina mpya nane za miche za zao la chai zinazohimili ukame, ukinzani na magonjwa, zenye tija nzuri ya uzalishaji na ubora wa vionjo vya kimataifa.

Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Taasisi za TARI na TRIT kwa kushirikiana na Kampuni ya Mbolea ya Minjingu inaendelea na majaribio ya mbolea ya Minjingu kwenye mashamba ya chai. Hatua nyingine ni kutoa mafunzo ya vitendo kwa wakulima 2,000 wa chai kupitia mashamba darasa 97 katika Halmashauri za Wilaya za Njombe, Rungwe na Mufindi kwa lengo la kuongeza tija, ubora na ushindani wa chai ya Tanzania kwenye masoko ya kimataifa.

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, Serikali imeendelea kuhamasisha wakulima wa chai kutumia umwagiliaji katika na baadhi ya wakulima chini ya makampuni ya Uniliver na DL wameanza kufanya majaribio ya matumizi ya mifumo ya umwangiliaji kwenye kukuza chai. Vilevile kupitia Mradi wa Agri-connect Serikali inaendelea na ujenzi wa miundombinu ya barabara kwa ajili ya kuendeleza mnyororo wa thamani wa mazao ya chai, kahawa na bustani katika Mikoa ya Ruvuma, Mbeya, Iringa, Songwe, Njombe na Katavi ambapo barabara zilizojengwa hadi kufikia Mei, 2021 zina urefu wa jumla ya kilometa 87.

Aidha, Mamlaka ya Mbolea Tanzania (TFRA) inaendelea kuhamasisha Vyama vya Ushirika katika zao la chai kutumia mfumo wa uagizaji wa mbolea bulk ambapo mwezi Februari Chama cha Ushirika wa Mazao na Masoko Mkonge kilifanikiwa kuagiza tani 500 mbolea aina ya NPK kwa ajili ya zao la chai.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuimarisha mfumo wa masoko ya chai na ifikapo Desemba, 2021 tutakuwa na mnada wa chai nchini Tanzania kwa mara ya kwanza ambao utafanyika Jijini Dar es Salaam na kutoa fursa kwa wazalishaji wakubwa na wadogo kushiriki kwenye uuzaji wa chai ndani ya nchi badala ya kupeleka chai kwenye mnada wa Mombasa nchini Kenya.