Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 52 Industries and Trade Wizara ya Viwanda , Biashara na Uwekezaji 437 2021-06-16

Name

Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Primary Question

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO aliuliza: -

Mihimili muhimu ya uchumi wa soko ni Mamlaka za Udhibiti, Tume ya Ushindani na Mamlaka ya kulinda haki na maslahi ya Watumiaji: -

(a) Je, ni lini Serikali itaunda mamlaka yenye nguvu ya kulinda haki na maslahi ya watumiaji nchini?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kutunga Sheria ya kuwalinda Watumiaji?

Name

Exaud Silaoneka Kigahe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Oscar Ishengoma Kikoyo, Mbunge wa Muleba Kusini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kumlinda Mlaji/Mtumiaji na inatekeleza jukumu hilo kupitia Sheria ya Ushindani Namba 8 ya Mwaka 2003 (The Fair Competition Act). Sheria hiyo ndiyo iliyounda Tume ya Ushindani (Fair Competition Commission – FCC) ambayo ndiyo mamlaka ya kuwalinda walaji/watumiaji wa bidhaa na huduma nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Sheria hii, Serikali imekamilisha uundaji wa Baraza la Kumtetea na Kumlinda Mlaji (National Consumer Advocacy Council) ambalo litakuwa na jukumu la kisheria kusimamia haki za mlaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kukamilisha taratibu za kuhakikisha Baraza hilo linaanzishwa ili liweze kujitegemea nje ya FCC, ili liweze kufanya kazi zake kwa ufasaha.

Aidha, Serikali inakamilisha maandalizi ya Sera ya Ubora ambayo pia ni muhimu katika kulinda haki za walaji/ watumiaji.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inazo sheria mbalimbali za kumlinda mlaji. Sheria hizo ni pamoja na Sheria ya Ushindani Namba 8 ya Mwaka 2003, Sheria ya Viwango ya Mwaka 1975, Sheria ya Vipimo ya Mwaka 1982, Sheria ya Usalama Mahali pa Kazi ya Mwaka 2003, Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 na Sheria ya Chakula, Madawa na Vipodozi ya mwaka 2003. Chini ya sheria hizo walaji mbalimbali hulindwa.