Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 46 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 382 2021-06-07

Name

Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Primary Question

MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza: -

Je, nini kinazuia kukamilika kwa ujenzi wa Barabara ya Makutano – Sanzate kwa kiwango cha lami ambayo ina miaka tisa sasa?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi kwa kiwango cha lami wa sehemu ya barabara kutoka Makutano hadi Sanzate yenye urefu wa kilometa 50, ulianza mwezi Mei, 2013 na ulitarajiwa kukamilika Mei, 2015. Ujenzi wa sehemu hii ya barabara, unatekelezwa na Kampuni ya Mbutu Bridge JV Contractors ambayo ni Muungano wa makampuni ya kizalendo 11 kwa gharama ya shilingi bilioni 46.1. Mbutu Bridge JV Contractors walipata mradi huu kwa njia ya ushindani baada ya kumaliza mradi wa mafunzo kwa Makandarasi Wazalendo wa Ujenzi wa Daraja la Mbutu ambao ulifanyika kwa ufanisi mkubwa. Hivyo, Serikali iliona ni fursa nyingine kwa kampuni ya kizalendo kuongeza uzoefu katika ujenzi wa barabara za lami.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuanza kwa utekelezaji wa mradi huu, kulijitokeza changamoto mbalimbali ikiwemo upatikanaji wa changarawe kwa ajili ya tabaka la barabara (G45), kuongezeka kwa kiasi cha upasuaji miamba na kuongezeka kwa kiasi cha ukataji udongo. Hali hii ilisababisha kubadilishwa kwa usanifu wa barabara na kulazimu Mkandarasi kuongezewa muda wa utekelezaji wa mradi hadi Februari, 2021.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Mkandarasi hakuweza kukamilisha kazi hiyo kwa muda uliopangwa. Kwa sasa kazi iliyobaki ni asilimia 12 maana yake imefanyika asilimia 88. Kufuatana na mpango mpya wa ujenzi, Mkandarasi amepanga kukamilisha ujenzi ndani ya miezi minne kuanzia sasa. Mkandarasi ameshapeleka katika eneo la kazi vifaa muhimu vya ujenzi ikiwa ni pamoja na malori, kokoto na lami.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali itahakikisha mapema iwezekanavyo baada ya kuhakiki madai ya mkandarasi shilingi bilioni 1.7 anazodai ili kumrahisishia kukamilisha kazi hii ndani ya muda nilioutaja. Ahsante.