Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 46 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 380 2021-06-07

Name

Boniphace Nyangindu Butondo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kishapu

Primary Question

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatatua migogoro ya mipaka kati ya Vijiji vya Mwanholo na Nyenze dhidi ya Mwekezaji na Mchimbaji Madini Eli Hilal Wilayani Kishapu?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nyangindu Boniphace Butondo, Mbunge wa Jimbo la Kishapu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua mgogoro wa mipaka kati ya Vijiji vya Mwanholo na Nyenze dhidi ya Mwekezaji na Mchimbaji wa Madini aitwaye Eli Hilal Wilayani Kishapu unaohusisha eneo lenye ukubwa wa hekta 2,872.4. Eneo hilo awali lililkuwa linamilikiwa na Mgodi wa Wiliamson Diamond Limited, kabla ya kugawiwa kwa Mchimbaji Eli Hilal ambaye alimilikishwa na Serikali. Baadhi ya wanakijiji wa Mwanholo na Nyenze hawaitambui mipaka ya eneo la mwekezaji wa uchimbaji wa madini na wengine wanalalamikia maeneo yao kutwaliwa na mwekezaji wa uchimbaji bila kulipa fidia.

Mheshimiwa Spika, mwezi Februari, 2021, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga iliunda Timu ya Wataalam kwa ajili kufanya uchunguzi wa mgogoro huo. Timu iliyoundwa imewasilisha taarifa yake na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga inaendelea kuifanyia kazi taarifa iliyowasilishwa ili kubaini masuala yanayoweza kushughulikiwa na Mkoa na yale yanayohitaji uamuzi wa ngazi za juu. Serikali kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga itashirikiana na wananchi na wadau wote muhimu katika kutatua mgogoro huu na kuhakikisha haki inatendeka.

Mheshimiwa Spika, ahsante.