Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 43 Industries and Trade Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara 364 2021-06-03

Name

Agnes Elias Hokororo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AGNES E. HOKORORO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itafufua Viwanda vya Korosho vilivyopo katika Wilaya za Masasi na Newala ili kuchakata korosho ghafi na kuongeza bei ya zao hilo?

Name

Exaud Silaoneka Kigahe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Agnes Elias Hokororo, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya za Masasi na Newala zilikuwa na viwanda vitatu vitatu vya kubangua korosho vilivyokuwa vikimilikiwa na Serikali na hatimaye kubinafsishwa. Viwanda hivyo ni Masasi Cashew Factory, Newala l Cashew Factory na Newala ll Cashew Factory.

Mheshimiwa Spika, Kiwanda cha Korosho cha Masasi kilichopo Masasi kilibinafsishwa na kuuzwa kwa Kampuni ya BUCCO Investments Holdings Limited ambayo ilishindwa kukiendeleza kutokana na Benki ya CRDB kuzuia mali za kiwanda baada ya kiwanda kushindwa kurejesha mkopo waliokopa. Hatimaye Kiwanda kiliuzwa na Benki ya CRDB kwa Kampuni ya Micronix Export Trading Co. Ltd kwa njia ya mnada. Kampuni ya BUCCO Investments Holdings Limited hawakuridhika na utaratibu uliotumika kuuza kiwanda hicho. Walifungua kesi mahakamani na kuishtaki Benki ya CRDB. Kesi hiyo bado ipo mahakamani hivyo uendelezaji wa kiwanda hicho umesimama kusubiri maamuzi ya Mahakama.

Mheshimiwa Spika, Kiwanda cha Newala I Cashew Factory kilinunuliwa na Kampuni ya Micronics System Ltd, kiwanda hiki kinaendelea kufanya kazi. Kiwanda cha Newala II Cashew Factory kilinunuliwa na Kampuni ya Agrofocus (T) Ltd. Tangu kibinafsishwe, Kiwanda hicho hakijawahi kufanya kazi. Hivyo, mwaka 2019 kilirudishwa katika umiliki wa Serikali chini ya Ofisi ya Msajili wa Hazina. Kiwanda hicho kama vilivyo viwanda vingine vilivyorudishwa Serikalini kipo katika utaratibu wa kupatiwa mwekezaji mwingine mwenye uwezo wa kukiendeleza.