Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 42 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 356 2021-06-02

Name

Rose Cyprian Tweve

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ROSE C. TWEVE aliuliza: -

Kumekuwepo na mkanganyiko wa tafsiri ya umri wa miaka 18 katika Sheria mbalimbali ikiwemo Sheria ya Mtoto na Sheria ya Kanuni za Adhabu na kupelekea kuvunja misingi ya Katiba: -

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuzifanyia mapitio Sheria hizo hususan kifungu cha 131 (2) ya Sheria ya Kanuni za Adhabu?

Name

Geophrey Mizengo Pinda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kavuu

Answer

NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rose Cyprian Tweve Mbunge wa Viti Maalumu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009, mtu aliye na umri chini ya miaka 18 anatambulika kuwa ni mtoto. Pamoja na kwamba kifungu cha 4(1) cha Sheria ya Mtoto kinabainisha kuwa mtoto ni mtu mwenye umri chini ya miaka 18, Kifungu cha 131(2) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu hakitoi tafsiri ya mtoto bali kinatoa adhabu kwa mtu mwenye miaka 18 au chini ya hapo anayekuwa na hatia ya kosa la kubaka na kupewa adhabu mbalimbali ikiwemo kuchapwa viboko kwa mkosaji wa mara ya kwanza, kufungwa jela kwa miezi 12 pamoja na viboko kwa mkosaji wa mara ya pili, au kifungo cha maisha kwa mkosaji kwa mkosaji anayejirudia kwa mara ya tatu. Kitaalamu hawa wanaitwa young offenders’ au wakosefu wenye umri mdogo.

Mheshimiwa Spika, Sheria zetu mbalimbali nje ya sheria ya Mtoto, zinaweka umri wa mtoto kulingana na muktadha na mazingira ya jambo mahsusi kama vile mikataba, jinai, kupiga kura, leseni za udereva na kadhalika. Kufuatia kutungwa Sheria ya Mtoto mwaka 2009, iliyotokana na Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Mtoto wa 1989 pamoja na masharti ya Ibara za Haki za ujumla za Binadamu kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977, na kwa kuwa Kifungu cha 131(2) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu kilifanyiwa marekebisho mwaka 2009 na baada ya kutungwa kwa Sheria ya Mtoto, ni dhahiri kuwa hakivunji misingi ya Katiba.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, Serikali sasa inapoendelea kuzipitia sheria mbalimbali, itakipitia pia kifungu hicho cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ili kufanya marekebisho kutokana na uhitaji uliopo kwa kuzingatia ushauri uliotolewa na Mheshimiwa Mbunge, ahsante.