Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 40 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 335 2021-05-31

Name

Regina Ndege Qwaray

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. REGINA N. QWARAY aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka na kuongeza vifaa tiba na wataalam katika vituo vya afya ilivyojenga vikiwemo vifaa tiba maalum kama vile “incubator beds” na taa maalum kwa ajili ya kukabiliana na homa ya manjano kwa watoto njiti?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Regina Ndege Qwaray, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika,utekelezaji wa mpango wa ujenzi wa vituo vya afya unaenda sambamba na mpango wa ununuzi wa vifaa tiba. Kuanzia mwaka wa fedha 2017/2018 hadi 2020/2021 Serikali imetoa jumla ya Shilingi bilioni 68.7 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika vituo vya afya vilivyojengwa na kukarabatiwa ili kuwezesha utoaji wa huduma za dharura na upasuaji kwa akinamama wajawazito na wananchi kwa ujumla. Vifaa vilivyonunuliwa vinajumuisha vifaa kwa ajili ya kusaidia watoto wanaozaliwa kabla ya muda (Infant Radiant Warmers).

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali imetoa shilingi bilioni 34 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika hospitali mpya 67 za Halmashauri zilizojengwa kuanzia mwaka wa fedha 2017/ 2018.

Mheshimiwa Spika, kuanzia Mei, 2017 hadi Mei, 2020 Serikali imeajiri na kuwapanga watumishi 9,531 wa kada mbalimbali za afya katika vituo vya kutolea huduma za afya nchini. Aidha, mwezi Mei 2021 Ofisi ya Rais - TAMISEMI imetangaza nafasi 2,726 za kada mbalimbali za afya. Wataalam hao watapangwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya kote nchini na kipaumbele kitakuwa kwenye vituo vyenye uhitaji mkubwa.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuboresha huduma za afya nchini kwa kuboresha miundombinu, kununua vifaa tiba na kuajiri wataalam wa kada mbalimbali za afya kwa kadri ya upatikanaji wa fedha, ahsante sana.