Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 36 Good Governance Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 296 2021-05-25

Name

Maida Hamad Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH aliuliza:-

Vipo baadhi ya Vijiji vilivyoorodheshwa kwa ajili ya kufikiwa na miradi ya TASAF III Awamu ya Kwanza upande wa Zanzibar lakini bado havijafikiwa na mradi unaelekea mwisho:-

Je, Serikali inasemaje juu ya maeneo ambayo hayajafikiwa na Mradi?

Name

Deogratius John Ndejembi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chamwino

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) naomba kujibu swali la Mhe. Maida Hammad Abdalla Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mradi wa TASAF haujafika mwisho na TASAF itafanya kila jitihada kuhakikisha kwamba kaya zinazotambuliwa na kuandikishwa kwenye mpango ni zile kaya maskini sana.

Mheshimiwa Spika, kipindi cha pili cha utekelezaji wa Mradi wa TASAF kimeanza baada ya uzinduzi uliofanyika tarehe 17 Februari, 2020. Zoezi la utambuzi na uandikishaji wa kaya za walengwa katika Vijiji/Mitaa/Shehia 5,590 ambazo hazikufikiwa na mpango wakati wa kipindi cha kwanza kimeanza tarehe 19 Aprili mpaka tarehe 6 Mei, 2021 kwa mzunguko wa kwanza.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Zanzibar jumla ya Shehia 304 tayari zinanufaika na mpango wa TASAF. Hata hivyo, jumla ya Shehia 157 ambazo hazikuwa kwenye mpango zimeshaandikishwa na ifikapo mwezi Julai, 2021 Shehia hizo zitaanza kunufaika na Mpango wa TASAF.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kuwasisitiza viongozi katika Vijiji/Mitaa na Shehia zote kutoruhusu vitendo vya upendeleo na kuingiza kaya ambazo hazina vigezo kwenye Mpango. Maeneo ambayo yatabainika kuwa na kaya zisizo na vigezo, viongozi watachukuliwa hatua za kinidhamu kwani watakuwa wamehusika kufanya udanganyifu na kuingiza wasiohusika kwenye Mpango. Naomba kuwasilisha.