Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 39 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 327 2021-05-28

Name

Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza:-

Halmashauri ya Wilaya ya Meatu imekumbwa na wimbi kubwa la uvamizi wa wanyamapori kwenye maeneo ya vijiji vinavyopakana na Pori la Akiba la Maswa na Hifadhi ya Wanyamapori Makao na kusababisha uharibifu wa mazao na kutishia usalama wa watu.

(a) Je, ni lini Serikali itashughulikia tatizo la uhaba wa watumishi wa Idara ya Wanyamapori?

(b) Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya ukosefu wa vitendea kazi vikiwemo gari na silaha?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, ninaomba kujibu Swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Meatu lenye sehemu
(a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Pori la Akiba la Maswa lililopo Mkoani Simiyu katika Wilaya za Bariadi, Meatu na Itilima limepakana na vijiji 32 ambapo vijiji 18 vipo katika Wilaya ya Meatu. Pori hilo lina ukubwa wa kilometa za mraba 274 na lilianzishwa mwaka 1974 kwa Tangazo la Serikali Na. 275. Mwaka 2016 usimamizi wa pori hilo ulihamishwa kutoka Idara ya Wanyamapori kwenda Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA) na wakati huo kulikuwa na watumishi 62.

Mheshimiwa Spika, kwa vipindi tofauti TAWA imechukua hatua za kuongeza watumishi kwa ajili ya kuimarisha usimamizi wa eneo hilo. Hadi kufikia Januari, 2021 pori hilo lina watumishi 87 sawa na ongezeko la asilimia 40 kutoka watumishi waliokuwepo mwaka 2016. Serikali inaendelea kuziba mapengo ya idadi ya watumishi kwa kadri ya upatikanaji wa vibali vya kuajiri watumishi. Vilevile Wizara itashirikiana na Ofisi ya Rais – TAMISEMI, kujenga uwezo wa Halmashauri kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, kuhusu ukosefu wa vitendea kazi, Wizara itaendelea kutenga fedha za ununuzi wa vitendea kazi ikiwemo magari na silaha ili kukabiliana na changamoto za wanyamapori wakali na waharibifu katika maeneo mbalimbali yakiwemo ya vijiji vinavyopakana na Pori la Akiba la Maswa.